USHAURI wa Rais John Magufuli, uliyomtaka Biswalo Maganga, Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DPP), kuangalia namna ya kuzungumza na watuhumiwa wa uhujumu uchumi na kuwaacha huru, imejibiwa vikali na Chadema. Anaripoti Hamis Mguta…(endelea).
Chama hicho kimeeleza kushtushwa na kauli hiyo, huku kikidai ushauri huo unatokana baadhi ya watuhumiwa kushikiliwa kwa makosa.
Tarehe tarehe 22 Septemba 2019, Rais Magufuli alimshauri Maganga, kwa kuzingatia sheria, kuangalia uwezekano wa kushughulika na watuhumiwa hao kama wapo tayari kurejesha fedha, basi wafanye hivyo.
Leo tarehe 24 Septemba 2019 kupitia tamko lao, Chadema kimedai, ushauri huo unatokana na ‘kusutwa’ na dhamira kwamba, baadhi ya waliokamatwa, walionewa.
Tamko la Chadema lililotolewa na Tumaini Makene, Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa chama hicho limeeleza, watuhumiwa hao wanastahili uhuru.
“…si tu imethibitisha madai ya kuwepo uonevu katika kile kilichoitwa vita dhidi ya ufisadi, bali pia inadhihirisha kuwa watuhumiwa hao wanastahili haki, uhuru wao bila masharti na waombwe samahani, badala ya wao kuomba,” limeeleza tamko hilo.
Tamko hilo limeeleza kwamba, mpaka sasa baadhi ya makosa ya watuhumiwa yameshindwa kuthibitishwa hivyo kusababisha kuendelea kuwa mahabusu kwa muda mrefu.
Chama hicho kimeeleza, kwa muda mrefu makundi mbalimbali yamekuwa yakilalama namna vita ya ufisadi kutowatendea haki baadhi ya watu.
“Hii inathibitisha kauli na madai ya watu na makundi mbalimbali katika jamii, ikiwemo Chadema yenyewe, ambayo mara kadhaa kupitia majukwaa mbalimbali, imetoa kauli kuwa vita iliyokuwa inaendeshwa na serikali, ililenga kuwaonea baadhi ya watu,” imedai sehemu ya taarifa hiyo.
Taarifa hiyo imeeleza wasiwasi kwamba, mpaka sasa baadhi ya watuhumiwa, hawajathibitishwa kuhusika na tuhuma hizo na kuhoji “watawezaje kukiri kuhusika kwenye tuhuma hizo?”
Leave a comment