RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli ametoa Sh. 15 bilioni kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa hospitali ya Rufaa ya Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere iliyojengwa kwa miaka 40 bila kumalizika mkoani Mara. Anaripoti Mwandishi wetu, Mara … (endelea).
Hayo yamebainika wakati wa ziara ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi katika hospitali hiyo kujionea maendeleo ya ujenzi wake.
Akizungumza mara baada ya kutembelea hospitali hiyo, Waziri Ummy amesema kuwa hospitali hiyo itakuwa msaada mkubwa kwa wananchi wa mkoa wa Mara hasa kwa huduma za matibabu ya kibingwa.
“Kutakuwa hakuna haja ya kwenda Hospitali ya Kanda Bugando kupata matibabu ya kibingwa kwani tunataka huduma za kibingwa zitolewe hapa hapa,” amesema.
Kwa upande wake Waziri Lukuvi amesema kuwa Shirika la Nyumba na Chuo Kikuu cha Ardhi kimepewa kazi ya kusimamia ujenzi wa hospitali hiyo hivyo ameagiza kazi kufanyika usiku na mchana ili limalizike kwa muda uliopangwa.
“Tumekubaliana tarehe 17 mwezi huu wa tatu, wawe wamekamilisha Wing C ili huduma za Mama na mtoto zinanze kutolewa kwa muda husika,” amesema.
Kwa upande wake Mkuu Mkoa wa Mara, Adam Malima amemshukuru Rais Magufuli kwa kutoa fedha kwa ajili ya kumalizia hospitali hiyo iliyokwama kwa muda wa miaka 40 mpaka sasa.
“Hospitali hii imechukua awamu tano za marais kumalizika na tunamshukuru Rais kwa kuchukulia kipaumbele katika hili,” amesema Malima.
Leave a comment