RAIS wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi amepokea kwa mshtuko na majonzi makubwa taarifa ya kifo cha shabiki maarufu wa Yanga, Ally Mohammed ‘Ally Yanga’, kilichotokea jana kwa ajali ya gari iliyotokea mkoani Dodoma, anaandika Yasinta Francis.
Katika salamu za rambirambi kwa uongozi wa Yanga, familia, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu Ally Yanga ambako Rais Malinzi amewaasa kuwa na moyo wa subira katika kipindi hiki kigumu kwao na kwa huzuni amewafariji akisema: “Sisi sote ni wa Mwenyezi Mungu, na kwake tutarejea.”
“Hakika nimeshtushwa na taarifa za kifo cha Ally Yanga ambaye nimejulishwa kuwa kilitokea katika ajali ya gari huko Dodoma. Kifo hiki kimefanya wanafamilia wa mpira wa miguu kupoteza hazina ya hamasa popote pale uwanjani.
“Binafsi nilimjua Ally Yanga katika masuala ya mpira wa miguu hasa akishabikia Yanga na timu zote za taifa bila kujali kuwa ni Twiga Stars (Timu ya taifa ya wanawake), Taifa Stars, Serengeti Boys au ile Ngorongoro Heroes,” amesema Malinzi na kuongeza:
“Hivyo, nawatumia Yanga salamu zangu za rambirambi nikiwapa pole kwa kuondokewa na mmoja wa mashabiki mwenye mvuto wa kipekee katika hamasa uwanjani, lakini pia alikuwa akisapoti timu za taifa.”
Aidha, Malinzi amesema: “Nawatumia pole wanachama wote wa Yanga kwa kuondokewa na shabiki mahiri Ally Yanga. Nawapa pole pia familia, ndugu, jamaa na marafiki ambao wamepoteza mhimili wao.
“Naungana nao katika msiba huu ambao pia ni msiba wetu sote wanafamilia ya mpira wa miguu. Naungana nao pia kumwomba Mwenyezi Mungu aiweke peponi roho ya Marehemu Ally Yanga. Amina.”
Leave a comment