PROFESA Ibrahim Juma, Jaji Mkuu wa Tanzania, amewataka wanasheria kuwa na fikra mpya katika Karne hii ya 21 kwa kuwa, mambo yamebadilika. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam … (endelea).
Amesema, fani nyingi zinafundisha masuala ya sheria hivyo uhitaji wa wanasheria umekuwa finywa, na kwamba ni wakati sasa wanasheria kuangalia fursa nyingine ili kukabiliana na maisha yao.
Prof. Juma ametoa kauli hiyo leo tarehe 10 Julai 2020, wakati wa kuwaapisha mawakili 161 wa Mahakama Mkuu.
“Tatizo kubwa tumeganda katika Karne ya 19 wakati dunia ipo Karne ya 21, na wanasheria wamekuwa wagumu sana kubadilika, nadhani litakuwa kundi la mwisho kubadilika.
“Nawasihi mawakili tuielewe Tanzania, tujaribu kuibua fursa, tuangalie uwekezaji wa SGR, umeme vjijini tusisite kuingia katika shughuli nyingine za kiuchumi ili kuongeza ushindani unaoendana na mabadiliko ya Karne ya 21,” amesema Juma.
Amesema, kutokana na maendeleo ya Teknolojia, baadhi ya mambo yamebadilika ikiwa ni pamoja na polisi kuwa na uwezo kufanya mahojiano kwa kupitia video.
“Sheria imebadilisha namna polisi wanavyoweza kufanya mahojiano kwa njia ya video ili kuondoa ubishani mahakamani, kuondoa usumbufu wa watuhumiwa kukana maelezo yao, matumizi ya TEHAMA hayakwepeki,” amesema.
Pia Prof. Juma amewataka mawakili hao walioapishwa leo, kuzingatia maadili na kusimamia mwongozo wa dira ya maendeleo ya Taifa.
Akitoa kisa kimoja cha mwanasheria wa Marekani, Prof. Juma amesema “mwanasheria mmoja wa Marekani alisema, sheria nyingi za Tanzania zina asili ya India za Karne ya 19, wakati uchumi wa Tanzania upo karne ya 21.
“Ndio maana wanasheria wanazidi kuachwa nyuma, TLS (Chama cha Wanasheria Tanganyika) wafanye utafiti kuona kama mitaala yetu inawafanya kuwa na ushindani,” amesema.
Pia amesema, kazi ya uwakili ni kazi ya kuaminiwa inayohitaji uaminifu wa hali ya juu, hivyo amewataka majaji hao kuwa na usiri unaoendana na taaluma yao.
“Unapompa huduma mwananchi, anakuamini na anakupa taarifa ambazo mara nyingi ni za siri, muwe waaminifu,” amesema Prof. Juma.
Leave a comment