Thursday , 28 March 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Jacob ajinadi Ubungo, agusia ushirikiano Chadema na ACT-Wazalendo
Habari za Siasa

Jacob ajinadi Ubungo, agusia ushirikiano Chadema na ACT-Wazalendo

Spread the love

BONIFACE Jacob, Mgombea Ubunge wa Ubungo kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) amesema, wako tayari kuachiana maeneo ya uchaguzi, kama watapata maelekezo ya viongozi wa chama chake kuhusu ushirikiano wa vyama vya upinzani kuelekea Uchaguzi Mkuu wa tarehe 28 Oktoba 2020. Anaripoti Regina Mkonde, Manzese … (endelea).

Jacob aliyekuwa Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo jijini Dar es Salam ametoa kauli hiyo leo Ijumaa tarehe 18 Septemba 2020 katika kampeni zake za ubunge, akiwa Mtaa wa Chakulabora Kata ya Manzese.

Amesema ili Jimbo la Ubungo liendelee kubaki upinzani wako tayari kushirikiana katika uchaguzi huo.

Jimbo hilo lilikuwa likiongozwa na Saed Kubenea kati ya mwaka 2015-2020 kupitia Chadema ambaye sasa anagombea Kinondoni jijini humo kupitia ACT-Wazalendo.

“Viongozi wakikubaliana wakitoa maelekezo sisi Ubungo tuko tayari kuyapokea. Naongea kwa dhati Ramadhani Kwangaya (Mgombea Udiwani Manzese kupitia  ACT-Wazalendo) anajua. Tuko tayari kushirikiana, wanasema wanataka kukomboa jimbo litoke  upinzani liende CCM, hilo haliwezekani Ubungo itaendelea kubaki upinzani,” amesema Jacob.

Mgombea huyo ubunge, alitoa kauli hiyo wakati anamnadi Hemed Ally Sabula, Mgombea Udiwani wa Manzese kupitia Chadema, ambapo alitumia nafasi hiyo kumzungumzia diwani aliyemaliza muda wake katika kata Ramadhani Kwangaya.

Kwanganya alishinda katika Uchaguzi Mkuu wa 2015 kupitia Chama cha Wananchi (CUF) baada ya vyama vilivyoshirikiana vya Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kuachiana nafasi ya urais, ubunge na udiwani.

Ukawa ilihusisha vyama vya Chadema, NLD, CUF na NCCR-Mageuzi.

Katika uchaguzi wa mwaka huu, kuna mazungumzo yanaendelea baina ya Chadema na ACT-Wazalendo yenye lengo la kushirikiana ili kusimamia mgombea mmoja wa urais, ubunge na madiwani kwa maeneo kadhaa.

Kuhusu uchaguzi huo, Jacob amewaomba wananchi wa Ubungo wamchague kwa kuwa ni mzawa wa jimbo hilo, hivyo anafahamu changamoto zao.

“Mimi ni mtoto wenu nimezaliwa hapa na kama mkinichagua maendeleo yakichelewa mna haki ya kusema mtoto wetu umekosea. Mama zangu, wazee wangu, kaka zangu, vijana ambao tumekua pamoja kwa miaka naomba mnichague. Msimchague mgeni, msichague kwa mkumbo,” amesema Jacob.

Amewataka wananchi wasirubuniwe na rushwa kutoka kwa wagombea bali wachague viongozi sahihi.

Akielezea ahadi zake, Jacob ameahidi kuondoa changamoto ya huduma za afya katika Kata ya Manzese kwa kuhakikisha zahanati iliyopo inapata watumishi wa kutosha, vifaa tiba na dawa ili ifanye kazi saa 24 kwa wiki.

Jacob ameahidi kuondoa changamoto ya Mto wa Ng’ombe kujaa takatakata zinazosababisha mafuriko yanayoathiri maisha ya wakati wanaoishi maeneo ya karibu na mto huo, pamoja na kuboresha sekta ya michezo.

“Wakati Wilaya ya Kinondoni inagawanywa nilipambana wilaya ya Ubungo ipate kijiko ambacho kitatumika kusafisha mto huu ili kuondoa changamoto ya mafuriko,” amesema Jacob.

Akielezea aliyoyafanya wakati alipokuwa Meya wa Ubungo, Jacob amesema, “Halmashauri ya Ubungo imekuwa halmashauri pekee iliyotenga Sh.3.4  bilioni kwa ajili ya mikopo ya kina mama na vijana hakuna halamshauri yoyote hata ya CCM imefanya, nikija kwenu kuna mambo nimefanya sio ya kuhadhithiwa.”

Jacob amesema katika uongozi wake wazee zaidi ya 30,000 waliwekwa katika mfumo wa kupata huduma ya afya bila malipo.

“Wazee zaidi ya 30,000 wanatibiwa bure, lakini si hilo tu, ukiweka jambo kubwa la kihistoria ndani ya Ubungo ingawa tunaambiwa fedha za wanawake, vijana na watu wenye ulemavu zimeanza kuchezewa kuna watu wamezila ushahidi upo mkinichagua nitaenda shughurikia,” amesema Jacob.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za SiasaTangulizi

CAG: Wastaafu, wenza wao chanzo NHIF kufilisika

Spread the loveRIPOTI ya ukaguzi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu...

Habari za SiasaTangulizi

Vikundi hewa 851 vyalamba bilioni 2.6 mikopo ya halmashauri

Spread the loveVIKUNDI hewa vya wajasirimali wadogo 851 kutoka katika halmashauri 19...

Habari za SiasaTangulizi

Mashirika matano yapata hasara mabilioni ya fedha

Spread the loveMASHIRIKA matano ya Serikali yanayojiendesha kibiashara, yamepata hasara ya mabilioni...

Habari za SiasaTangulizi

CAG aibua madudu halmashauri 10, TANESCO na MSD

Spread the loveRIPOTI ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali...

error: Content is protected !!