IKULU ya Tanzania imesema kuwa majadiliano baina ya Kamati maalumu ya Tanzania na wawakilishi kutoka kampuni ya Barrick Gold Corporation unaendelea hadi sasa ikiwa ni siku ya 15,anaandika Irene Emmanuel.
Majadiliano hayo yanafanyika katika ukumbi wa mikutano wa Ikulu, jijini Dar es Salaam, yalitarajiwa kuchukua muda mfupi lakini yameendelea mpaka sasa huku ikiwa haijulikani ni lini yatamalizika.
Upande wa Tanzania unaongozwa na Profesa Palamagamba Kabudi, Waziri wa Katiba na Sheria, huku Barrick wakiongozwa na Richard Williams, Ofisa Mwendeshaji Mkuu.
Ukimya mkubwa kuhusu majadiliano hayo ulisababisha MwanaHALISI online imtafute Gerson Msigwa, Mkurugenzi wa mawasiliano Ikulu.
“Majadiliano bado yanaendelea chini ya Prof. Kabudi,” amesema kwa kifupi.
Akitoa maoni yake kuhusu mazungumzo hayo, Halima Mdee, Mbunge wa Kawe, amesema; “Ukimya huu unanipa shaka na kujiuliza hivi majadiliano ya Acacia yanaendelea au washarudi kwao? Mbona yanaendeshwa kwa kificho kikubwa na taarifa za walipofikia hazitolewi?”
Hashimu Rungwe, Mwenyekiti wa Chama cha Ukombozi wa Umma (Chaumma), amesema huenda taarifa kuhusu mazungumzo hayo hazitolewi kwasababu ya takwimu zisizo za kweli zilizotolewa na kamati mbili za Rais tofauti na uhalisia wa mambo.
Mazungumzo yanayoendelea ni zao la uchunguzi wa kamati mbili maalum za kuchunguza mchanga wa madini (makinikia) kwenye makontena 277, yaliyozuiwa bandarini.
Ripoti zilieleza kuwa kuanzia mwaka 1998 mpaka sasa Tanzania imepoteza jumla ya Sh. 108.46 trilioni katika sekta ya madini kutokana na udanganyifu wa makampuni ya madini.
Leave a comment