MKUU wa jeshi la polisi nchini (IGP), Simon Sirro, ametangaza mabadiliko ya makamanda wa mikoa katika jeshi lake kwa kuhamisha baadhi huku na kupeleka kule. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea).
Miongoni mwa waliohamishwa, ni pamoja na aliyekuwa Kamanda wa polisi mkoa wa Mwanza, Naibu Kamishena, Ahmed Msangi ambaye ameletwa makao makuu ya upelelezi jijini Dar es Salaam.
Msangi amefanywa kuwa mkuu wa kitengo cha makosa dhidi ya binadamu.
Taarifa ya mabadiliko hayo imetolewa leo tarehe 15 Agosti 2018 na msemaji wa jeshi hilo, Kamishena msaidizi wa polisi, Barnabas Mwakalukwa.
“Uhamisho huo ni mabadiliko ya kawaida yanayotokea ndani ya Jeshi la Polisi katika kuongeza ufanisi wa utendaji kazi,” inaeleza sehemu ya taarifa hiyo.
Sehemu ya taarifa hiyo pia imeeleza kuwa nafasi ya DCP Msangi, imechukuliwa na aliyekuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Jonathan Shana.
Naye aliyekuwa mkuu wa operesheni Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Wankyo Nyigesa, amechukua nafasi ya Shana.
Leave a comment