UNYAMA na vitendo vya ukiukwaji wa sheria vimelalamikiwa na Mhandisi Hamad Massauni, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Waziri Massauni ameeleza kukithiri kwa vitendo hivyo mahabusu, huku akitolea mfano kisa cha mwanamke na mtoto wake wa mwaka mmoja na nusu, waliosota mahabusu kwa mwaka mmoja na nusu.
Ameeleza kisa hicho wakati akizungumza na vyombo vya habari, kuhusu ziara yake aliyoifanya ya kutembelea mahabusu ili kujua changamoto wanazokabiliana nazo.
Akieleza kisa hicho amesema, mwanamama huyo na kichanga chake, waliwekwa mahabusu, akituhumiwa kuiba kitenge chenye thamani ya Sh. 30,000.
Mhandisi Massauni ameeleza kuwa, kilichosababisha changamoto hiyo ni mamlaka husika kutowajibika ipasavyo, huku akiinyooshea kidole Kamati za Kuharakisha kesi nchini.
“Kwa sababu ya kutowajibika kwetu ipasavyo, naomba nitoe mfano mmoja, nilimkuta msichana mmoja ana mtoto mdogo wa mwaka mmoja na nusu yuko zaidi ya miezi mitano katika mahabusu, lakini hajawahi kupelekwa mahakamani. Na uhakika angepelekwa mahakamani, siku ya kwanza tu hakimu angempa dhamana, “ amesema Mhandisi Massauni na kuongeza.
“Kosa mume wake alikuja na kitenge nyumbani kwake yeye akavaa akakamatwa, akaambiwa ameiba kitenge cha 30,000. Mtu kama huyu mnamuweka gerezani miezi mitano hadi sita, halafu hakuna mtu anayeguswa kwa hili jambo kuchukua hatua za haraka.”
Leave a comment