WAZIRI wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amesema, Serikali imerudisha huduma za kawaida katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dar es Salaam Amana kwa sababu hakuna tena mgonjwa wa COVID-19. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam…(endelea).
Waziri Ummy ameyasema hayo jana Alhamisi tarehe 18 Juni 2020 wakati akizindua Kituo cha Taifa cha Huduma za Tiba Mtandao ambacho kitakuwa katika kituo cha MOI Muhimbili.
Alisema, katika mkoa wa Dar es Salaam nzima kwenye hospitali za serikali na binafsi kuna wagonjwa wawili tu wa virusi vya corona.
Pia, katika Hospitali ya Mloganzila ambayo ilikuwa miongoni mwa hospitali iliyokuwa ikihifadhi wagonjwa wa corona napo hakuna mgonjwa hivyo Serikali imeamua kurudisha huduma hizo katika hospitali ya Amana ambayo pia iliteuliwa kuhudumia wagonjwa wa ugonjwa huo pekee.
“Pamoja na kuwa maambukizi ya ugonjwa wa corona yanapungua, Mganga mkuu wa serikali, kubwa ambalo tunalisisitiza kama sekta ya afya, lazima mgonjwa na mtumishi kuvaa barakoa.”
“Kwetu sisi sekta ya afya, kuibuka kwa ugonjwa wa corona kunatakiwa kuona fursa ya kuimarisha kanuni za udhibiti wa maambukizi katika vituo vya kutoa huduma ya afya,” alisema
“Ni maelekezo yangu Mganga Mkuu wa Serikali waandikie waganga wakuu wa mikoa yote, vituo vya kutoa huduma za afya vya serikali na binafsi, mtumishi, mgonjwa na mtu anayeenda kumuona mgonjwa lazima wavae barakoa,” amesema Ummy.
Hata hivyo, ameeleza kuwa watu ambao hawana mawasiliano ya karibu sana ama mgusano wa moja kwa moja na mgonjwa watatakiwa kuvaa barakoa za vitambaa ili kujikinga bila kusahau suala la kunawa mikono kwa maji tiririka na sabuni.
“Lazima tulizingatie, waganga wakuu wa mikoa piteni kwenye vituo vyote vya kutoa huduma za afya muhakikishe haya yanafanyika, tunaendelea kuhimiza kukaa kwa umbali wa mita moja, kwasababu tunataraji kutokomeza ugonjwa huu wa Corona Tanzania lakini hili lisitufanye tukabweteka,” alisema.
Aidha, Waziri Ummy alisema, corona imetoa fursa ya kutoa huduma ya tiba mtandao nchini ambapo Rais wa Tanzania, John Magufuli ameibeba sekta ya afya katika kipindi cha utawala wake.
Leave a comment