Wednesday , 24 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Hoja tano za muungano Tanzania zafutwa
Habari za Siasa

Hoja tano za muungano Tanzania zafutwa

Rais Samia Suluhu Hassan
Spread the love

SERIKALI ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imefuta hoja tano za muungano wa Tanganyika na Zanzibar zilizopatiwa ufumbuzi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).

Leo Jumamosi tarehe 17 Oktoba 2020, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SMT) na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), zimesaini hati za makubaliano ya kuondoa hoja hizo Ikulu jijini Dar es Salaam.

Shughuli hiyo imetekelezwa na mawaziri na wanasheria wa SMT na SMZ na kushuhudiwa na Makamu wa Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan na Makamu wa Pili wa Rais wa SMZ, Balozi Seif Ali Idd.

Hoja zilizofutwa ni Ushirikishwaji wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), katika masuala ya kimataifa na kikanda. Ushirikishwaji wa SMZ katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, gharama ya kushusha mizigo katika bandari ya Dar es Salaam inayotoka Zanzibar.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa

Nyingine ni, utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi na utaratibu wa vikao vya Kamati ya Pamoja na Serikali ya Muungano wa Tanzania na SMZ.

Hoja ya kwanza iliyofutwa ni ushirikishwaji wa SMZ katika masuala ya kimataifa.

Akifafanua utatuzi wa hoja hizo, Balozi Joseph Sokoine, Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira amesema, msingi wa hoja hiyo ilikuwa ni Wizara ya Mambo ya Nje ya Tanzania kutoipa nafasi ya kutosha Zanzibar ya kuwa na ushirikiano wa kiuchumi unaohitajika kwenye taasisi za kimataifa.

Prof. Palamaganda Kabudi, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

“Ufumbuzi, Serikali ya SMT na SMZ zimetayarisha muongozo wa ushirikishwaji wa SMZ katika masuala ya kimataifa na kikanda iliyozingatia ziara ya viongozi wa kitaifa, mikutano ya kimataifa, nafasi za masomo ya elimu ya juu nje ya nchi.”

“Utafutaji fedha za misaada au mikopo ya kutekeleza miradi mbalimbali ya nje ya nchi, muongozo huu uliridhiwa na kamati ya pamoja inayoshughulikia masuala ya muungano,” amesema Balozi Sokoine.

Hoja ya pili, ni ushiriki wa SMZ katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, ambapo zoezi hilo limetekelezwa na Waziri wa Nchi ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la SMZ, Issa Ussi Gavu chini ya Wanasheria Wakuu wa Serikali hizo Prof, Adelardus Kilangi (SMT) na Said Hassan Said (SMZ).

Malalamiko katika hoja hiyo ilikuwa ni nafasi ya Zanzibar katika kuwasilisha miradi ya maendeleo ya kiuchumi, kwa ajili ya kujumuishwa kwenye miradi ya kikanda katika jumuiya hiyo.

Mussa Zungu, Waziri wa Ofisi ya Makamo wa Rais Muungano

Balozi Sokoine amesema, ufumbuzi wake ni SMZ kuwasilisha miradi nane ya maendeleo kwa ajili ya kujumuishwa katika miradi ya kikanda inayowasilihwa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Ambapo miradi minne ilipewa kipaumbele kwa ajili ya kuombewa fedha za utekelezwaji, ikiwemo mradi wa ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Pemba.

Hoja ya tatu, iliyofutwa ni gharama za kushusha mizigo katika Bandari ya Dar es Salaam inayotoka Zanzibar, hati za kufuta hoja hiyo ilisainiwa na Waziri wa Viwanda na Biashara wa Tanzania, Innocent Bashungwa na Waziri wa Viwanda, Biashara na Masoko Zanzibar, Balozi Amina Salum Ali.

Hoja ya nne, iliyofutwa ni utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia Zanzibar, ambapo msingi wake ilikuwa ni namna ya kugawana mapato ya rasilimali hizo zitakapo patikana, ambapo Serikali zote zilijadiliana kwa kutumia mshauri mwelekezi wa masuala ya mgawany wa rasimali za mafuta na gesi asilia.

Balozi Soikone amesema, ufumbuzi wa hoja hiyo ilikuwa ni suala la mafuta na gesi asilia kuondolewa katika orodha ya masuala ya muungano, na kwamba Zanzibar imepatiwa mamlaka yakusimamia sekta hizo na kuanzisha vyombo vya kusimamia mafuta na gesi asilia.

Hoja ya mwisho iliyofutwa ni utaratibu wa vikao vya Kamati ya Pamoja na Serikali ya Muungano wa Tanzania na SMZ, ambapo ufumbuzi wake ulikuwa ni uanzishwaji wa taratibu za vikao vya kamati ya pamoja ya SMT na SMZ kushughulikia masuala ya hoja za muungano.

Aidha, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mussa Zungu amesema, hoja nyingine sita za muungano zimetafutiwa ufumbuzi na kwamba zinasubiri kupata ridhaa ya Kikao cha Kamati ya pamoja ya Serikali ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ).

“Pamoja kwamba leo tunaondoa hoja tano katika orodha ya hoja za muungano, naomba kuchukua fursa hii kueleza hoja nyingine sita zimeatiwa ufumbuzi zinasubiri kupata ridhaa ya kikao cha kamati ya pamoja ya SMT na SMZ kama ilivyoanishwa katika utaratibu wa pamoja,” amesema Zungu.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

Kilosa yawa mfano wa kuigwa miradi ya Mwenge nchini

Spread the love  KIONGOZI wa Mbio za Mwenge Kitaifa Godfrey Mzava amezitaka...

Habari za SiasaTangulizi

Biteko ataja vipaumbele 7 bajeti nishati 2024/25

Spread the love  NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto...

Habari MchanganyikoHabari za Siasa

Mwekezaji amwaga bil. 39 kujenga viwanda 3 vya uchenjuaji

Spread the loveKampuni ya Mineral Access System Limited (MAST) inayoiwakilishwa kampuni ya...

Habari za SiasaTangulizi

Mpwa wa Magufuli mbaroni kwa kusambaza picha za utupu

Spread the loveJESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limewakamata...

error: Content is protected !!