KUFUATIA kiapo cha kisasi kilichowekwa na Irani dhidi ya Marekani, baada ya Meja Jenerelali Qasem Soleiman, kiongozi wake mwandamizi wa Jeshi kuuawa, Wamarekani waishio nchini Tanzania watahadharishwa. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Leo tarehe 6 Januari 2019, Ubalozi wa Marekani nchini Tanzania, umewataka raia wake waishio hapa nchini, kuwa makini.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na ubalozi huo kupitia ukurasa wake wa Twitter, mvutano huo ulioibuka kwenye nchi za Mashariki ya Kati, unaweza kusababisha athari za kiusalama kwa raia wa Marekani waishio nje ya taifa lao.
Ubalozi huo umewataka raia wake kuwa makini katika maeneo yao, pamoja na kuandaa nyaraka zao za usafiri.
“Ubalozi utaendelea kutoa taarifa kadri itakavyohitajika. Mnachotakiwa kufanya kuwa makini na mazingira yanayowazunguka, kupitia upya mipango yenu ya usalama pamoja na kuandaa ama kuhuisha nyaraka zenu za usafiri, na kuziweka maeneo ambayo itakuwa rahisi kupatikana,” inaeleza taarifa ya ubalozi huo.
Mzozo wa Irani na Marekani umeibuka kufuatia kifo cha Jenerali Soleiman, kilichotokea Ijumaa ya tarehe 3 Januari 2020, mjini Baghdad nchini Iraqi.
Hadi sasa mataifa hayo mawili yametambiana kulipiza kisasi, ambapo Rais wa Marekani Donald Trump ametangaza kuchukua hatua kali kwa Irani, itakapothubutu kulipa kisasi. Huku Irani ikitangaza dau nono la Dola za Marekani 80 milioni, kwa mtu atakayefanikiwa kupata kichwa Trump.
Nchi ya Iraqi alipouawa Jenerali Soleiman, imepitisha azimio la kuondoa wanajeshi wa kigeni, huku walengwa ikiwa ni wanajeshi wa Marekani.
Kufuatia hatua hiyo, Rais Trump ameendelea kutoa vitisho, akitangaza kuiwekea vikwazo pamoja na kufanya mashambulizi Iraqi, ikiwa itatekeleza mpango huo.
Leave a comment