UONGOZI wa klabu ya Yanga amesema uuzaji wa jezi feki ni moja ya kitu kinachowapa Yanga unyonge kutokana na kukosa mapato na kunufaika watu wengine. Anaripoti Kelvin Mwaipungu … (endelea).
Msemaji na Afisa Uhamasishaji wa klabu hiyo, Antonio Nugaz amesema kuwa mpaka sasa wana taarifa ya kontena moja limeshaingia bandarini ambalo limesheheni jezi feki na wapo kwenye hatua ya mwisho za uchunguzi ili kujua wahusika ni wakina nani kabla ya kwenda kulikamata.
“Moja kati ya taarifa ambayo ipo ni kwamba kuna kontena limeingizwa lina jezi janjajanja (feki) kwa hiyo wanalifuatilia kwa kina ili kujua kampuni iliyoagiza na nani kahusika ili itakapotimia tukienda kuvamia tupate kitu sahihi.
“Hiki kinasababisha Yanga kuwa nyonge sana, hii ndiyo sehemu ambayo pato la timu linaweza kuwa sawa na timu ikaweza kujiendesaha kwa kutegemea mauzo ya jezi,” amesema Nugaz.
Hivi karibuni kampuni ya GSM ambayo inadhamana ya kuuza vifaa vya Yanga kwa kushirikiana na klabu hiyo iliweza kufanya msako wa kukamata jezi feki kwenye soko la K/koo na kufanikiwa kukamata jezi zaidi ya 1,000 ambazo zilikuwa kinyume na utaratibu.
Aidha uongozi wa klabu hiyo umesema kuwa zoezi hilo ni endelevu wakishirikiana na GSM huku wakitoa rai kwa mashabiki wa klabu hiyo kununua jezi kwenye sehemu husika na siyo chini ya miti kama ilivyozoeleka.
Leave a comment