BODI ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HESLB), imesema haitatoa nafasi ya wanafunzi waliokosea kuomba mikopo kurekebisha makosa yao, kama ilivyoombwa na wanafunzi pamoja na wadau mbalimbali wa elimu, anaandika Charles William.
Katika mahojiano na MwanaHALISI Online, Cosmas Mwaisobwa, Mkurugenzi Msaidizi wa Habari, Elimu na Mawasiliano wa HESLB amesema, kila mwanafunzi anao wajibu wa kuhakiki taarifa za maombi yake kabla ya kuwasilisha maombi hayo.
“Mwanafunzi akishajaza taarifa zake zote na aka’submit (kuwasilisha) maombi yake, maana yake amejiridhisha na taarifa alizojaza. Sasa ukiniambia anataka kurekebisha, hakutakuwa na huo utaratibu,” amesema Mwaisobwa.
Wito wa kuwepo kwa muda wa wanafunzi kurekebisha makosa katika maombi yao ya mikopo, ulitolewa na Mtandao wa wanafunzi Tanzania (TSNP), kwa hoja kuwa, wanafunzi wengi wamekumbana na changamoto katika uombaji wa mikopo kupitia mfumo mpya – mtandaoni.
“Kuna changamoto nyingi wanafunzi wanaoomba mikopo wamekumbana nazo, tunaomba HESLB itoe majina ya waliokosea kujaza ili waweze kurekebisha makosa hayo, katika muda wa nyongeza uliotangazwa,” alisema Abdul Nondo, Kaimu Mkurugenzi wa haki na wajibu wa wanafunzi TSNP.
Hata hivyo, Mwaisobwa amesema, “mfumo wetu unaonesha kipi mwanafunzi amekikamilisha na kipi bado. Kama mtu ameweka cheti cha kidato cha nne, halafu hajaweka cha kuzaliwa, anaoneshwa aweke ili maombi yake yakamilike ndipo anawasilisha kwetu. Hakutakuwa na utaratatibu wa mtu kurekebisha.”
Itakumbukwa kuwa, katika miaka ya nyuma HESLB ilikuwa ikitoa majina ya wanafunzi wanaokosea kujaza fomu za maombi ya mikopo. Mathalani, Oktoba Mosi, 2016 bodi ilitangaza majina ya waombaji wa mikopo 2016/2017 waliokosea na kutoa muda mpaka tarehe 7 Oktoba, 2016 wanafunzi hao warekebishe makosa.
Katika hatua nyingine Mwaisobwa, amefafanua kuwa fedha ya kujikimu itaendelea kuwa Sh. 8500 kwa siku, kwa mwanafunzi atakayepata mikopo na kusema, bodi haikuweka kiwango hicho katika muongozo wa mwaka huu kwani hakuna mabadiliko.
HESLB inatarajia kutoa mikopo kwa wanafunzi wapya 30,000 katika mwaka wa masomo 2017/2018, ambapo mpaka sasa zaidi ya wanafunzi 38,000 wameomba mikopo na zoezi likiendelea mpaka tarehe 11 Septemba, 2017.
Leave a comment