JOB Ndugai, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amesema kuwa bado anaitafakari barua ambayo ameipokea kutoka kwa, Ibrahim Lipumba, Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF) ambaye anatambulika na msajili wa vyama vya siasa, anaandika Hellen Sisya.
Katika taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari mapema leo hii, Ndugai amethibitisha kupokea barua kutoka kwa Lipumba kumtaarifu kuhusiana na uamuzi wa Baraza kuu la chama hicho wa kuwafukuza uanachama baadhi ya wabunge na madiwani kutokana na makosa kadhaa ya kinidhamu.
Ndugai amesisitiza kuwa suala la kuwaondoa uanachama ni la utashi wa vyama husika na kila chama kina utaratibu wake, hivyo bado anaitafakari hiyo barua na maamuzi yake kwa wabunge waliofukuzwa uanachama atautoa baadae.
Wabunge waliotajwa kufukuzwa uanachama ni pamoja na Severina Silvanus Mwijage, Saumu Sakala, Salma Mwassa, Riziki Ngwali, Raisa Abdallah Mussa, Miza Bakari Haji, Hadija Ally Al-Qassmy, Halima Ali Mohamed.
Mgogoro ndani ya Chama cha CUF ulianza wakati ambapo Lipumba alipoamua kujiuzulu nafasi ya uenyekiti aliyokuwa nayo na kubaki kuwa mwanachama wa kawaida baada ya Chama hicho kikishirikiana na vyama vingine vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) kumteua Edward Ngoyai Lowasa, waziri mkuu mstaafu kuwa mgombea wao wa nafasi ya urais kwa mwaka 2015.
Leave a comment