ZACHARIA Hans Pope, Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Klabu ya Simba amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na kuunganishwa kwenye kesi ya utakatishaji fedha inayowakabili vigogo wa klabu hiyo. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Pope pamoja na Mfanyabiashara anayefahamika kwa jina la Franklin Lauwo wamefikishwa leo tarehe 16 Oktoba 2018 katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, ambapo wataungana na Rais wa Simba, Evans Aveva na Makamu Mwenyekiti wa Klabu hiyo, Geofrey Nyange katika kesi ya kughushi nyaraka feki na utakatishaji fedha.
Hapo awali TAKUKURU kupitia mkurugenzi wao mkuu Jenerali John Mbungo walisema kuwa Hans Pope alitoa taarifa TRA kuwa Simba ilinunua nyasi kutoka nchini China kwa kiasi cha dola za kimarekani 45,577, sawa na pesa za kitanzania Sh. 105 milioni, kumbe uhalisia walinunua kwa Dola 109,499, sawa na Sh. 252 milioni.
“Nia yake ilikuwa ni kutolipa mapata yanayotakiwa na TRA na kwa mujibu wa sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa nchini hilo ni kosa na walijaribu kumtafuta kwa njia ya uwazi ili aje ajibu tuhuma hizo.” Alisema Mbungo.
Hans Pope alikamatwa juzi tarehe 14 Oktoba 2018 katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) akitokea Marekani alipokuwa kwenye matibabu.
Leave a comment