HALIMA Mdee,Mbunge wa Kawe na Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake Chadema (BAWACHA), amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na kusomewa shtaka la kutumia lugha ya matusi, anaandika Irene David.
Mdee baada ya kushikiliwa kwa siku sita zilizopita kwa amri ya Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni,Leo ameachiliwa kwa dhamana ya Sh.10 milioni.
Mbunge huyo alifikishwa katika hiyo mbele ya Hakimu Mkazi, Victoria Nongwa ambapo upande wa serikali uliwakilishwa na Wakili wa Serikali, Nasoro Katuga.
Baada ya kusomewa mashtaka hayo, Hakimu Victoria amesema dhamana ipo wazi na Mdee amedhaminiwa na wadhamini wawili kwa bondi ya Sh. 10 milioni kwa kila mmoja na yeye mwenyewe.
Mdee amepata dhamana na yupo nje kwa dhamana mpaka Agosti 7, 2017 kesi hiyo itakapotajwa tena.
Baada ya kuhairishwa kwa kesi hiyo, Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa Chadema, amewaambia waandishi wa habari kuwa kauli iliyotolewa na Halima Mdee ni msimamo wa chama wa kupinga kauli za rais zinazokinzana na katiba ya Tanzania.
“Mdee ni mbunge, pia ni Mwenyekiti wa Bawacha, ni kiongozi mwandamizi na hivyo licha ya kusema tu bali pia ana haki ya kukemea sababu ni moja ya majukumu yake,” amesema Mbowe na kuongeza:
“Kila mtanzania bila kujali kabila, dini na chama anahaki ya kusema hisia zake. Chama kitaendelea kuzungumzia kauli za rais bila kujali polisi watatumia sheria gani.”
Leave a comment