MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu imeuitaka Jamhuri kukamilisha upelelezi wa kesi ya uhujumu uchimi inayomkabili mfanyabiashara Yusuf Manji, anaandika Faki Sosi.
Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama hiyo, Thomas Simba amesema kuwa upande wa mashtaka upelelezi ukamilishwe haraka ili matokeo ya kesi hiyo yajulikane.
Leo mahakamani hapo wakili wa serikali, Wankyo Simon aliomba tarehe ya kutajwa kwa kesi hiyo na kwamba upelelezi wa kesi hiyo haujakamilika.
Hata hivyo wakili utetezi aliutaka upande wa Serikali kueleza hatua waliyofika kwenye upelelezi huo. Kesi hiyo imeaihirishwa mpaka Agosti 31 mwaka huu.
Awali mfanyabiashara huo alisomewa mashtaka manane akiwa amelazwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.
Manji (41) na wenzake, wanadaiwa kukutwa na vitambaa vyenye thamani ya Sh200 milioni, vinavyotumika kutengeneza sare za Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ). Pia, wanadaiwa kukutwa na mihuri.
Wanashtakiwa chini ya Sheria ya Uhujumu Uchumi na Sheria ya Usalama wa Taifa. Washtakiwa wengine ni Deogratius Kisinda (28), Abdallah Sangey (46) na Thobias Fwere (43).
Walisomewa mashtaka hayo ndani ya wodi aliyolazwa Manji na wakati yakisomwa, Manji alikuwa amevaa sare za bluu za wagonjwa na alikuwa ameketi kitandani huku mkononi akiwa ametundukiwa dripu.
Leave a comment