ASKOFU Josephat Gwajima, mgombea ubunge katika Jimbo la Kawe kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), amesema alianza kuitumikia Kawe siku nyingi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Amesema, kabla ya kuwa mbunge, tayari wakazi wa Salasala 250 na misikiti saba imeneemeka kwa kuunganishia maji kwa fedha zake mwenyewe.
Na kwamba, kazi ya ubunge anayoimba kutoka kwa wananchi, si ya kuganga njaa bali kuwatumikia wananchi wa jimbo hilo tu.
Akizungumza kwenye kampeni zake katika Kata ya Kawe, mgombea huyo amesema hatosubiri fedha za serikali kufanya maendeleo kwenye jimbo hilo bali ataingia mfukoni kwake.
“Mimi sijaja kufanya kazi hii kuganga njaa” amesema Gwasjima na kuongeza “acha hao wa upande ule ambao wanaomba ubunge kutumia fedha waliyokopa benki.”
Askofu Gwajima amesema, atanunua greda na maroli kwa kutumia fedha zake kwa ajili ya kukarabati barabara za mitaa yote ya jimbo la Kawe.
Ameahidi kununua magari ya wagonjwa ambayo yatahudumia jimbo hilo na kwamba, wapo
wabunge ambao aliwasaidia kununua magari 18 ya namna hiyo na kuwakabidhi kwa ajili ya majimbo yao.
“Ununuzi wa magari haya kwangu ni jambo dogo sasa,” amesema Askofu Gwajima huku akisisitiza atasambaza magari hayo ndani ya jimbo hilo kwa siku 90 baada ya kuchaguliwa.
Askofu Gwajima alitoa ahadi hizo juzi wakati akizungumza na wanachama wa CCM na wananchi wa Kata ya Kawe alikokuwa anaendelea na mikutano yake ya kampeni.
Leave a comment