MUDA mchache baada ya kusambaa kwa taarifa katika mitandao ya kijamii juu ya kukamatwa kwa Askofu Josephat Gwajima wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Simon Sirro Kamishna wa Polisi Kanda Malum ya Dar es Salaam amesema bado hana taarifa juu ya suala hilo, anaandika Charles William.
Mapema leo mchana zilisambaa taarifa katika mitandao ya kijamii kuwa Jeshi la Polisi jijini Dar limemkamata Askofu Gwajima nyumbani kwake na kumfanyia upekuzi na kwamba baada ya kumpekua limempeleka Kituo cha Polisi cha Kati.
Hata hivyo, taarifa hiyo katika mitandao ya kijamii haikufafanua zaidi kuwa, Askofu Gwajima amekamatwa kwa tuhuma gani na amepekuliwa nyumbani kwake kwa lengo la kutafuta ushahidi gani.
Hata hivyo, mtandao huu ulipomtafuta Kamishna Sirro, amejibu kwa kifupi “Mimi bado sina taarifa za jambo hilo, ngoja nifuatilie.”
MwanaHALISI Online imemtafuta Askofu Gwajima kwa njia ya simu, hata hivyo hakupatikana.
Askofu Gwajima aemkuwa katika mvutano na Paulo Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam tangu Makonda alipomtuhumu kujihusisha na dawa za kulevya na hivyo kushikiliwa na jeshi la polisi kwa siku mbili na kuhojiwa kabla ya kuachiwa.
Jumapili iliyopita Gwajima alijibu mapigo kwa kusema Makonda alimtaja yeye kutokana na hofu kuwa Askofu huyo anaweza kuwania ubunge katika Jimbo la Misungwi, Mwanza ambalo hata RC huyo anajipanga kugombea.
Alienda mbali na kusema jina halisi la Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam ni Daudi Albert Bashite na kwamba jina lake la sasa limetokana na kuchukua cheti cha kidato cha nne cha mtu anayejulikana kama Paulo Christian.
Leave a comment