WAJUMBE wa mkutano mkuu wa jimbo la Vunjo Mkoa wa Kilimanjaro wamempendekeza, mbunge wa viti maalum (Chadema), Grace Kiwelu kupeperusha bendera ya ubunge wa jimbo la vunjo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kilimanjaro…(endelea)
Grace alibuka mshindi katika mkutano wa kura za maoni zilizofanyika jana Jumanne tarehe 14 Julai 2020 katika jimbo hilo linaloongozwa na James Mbatia wa NCCR-Mageuzi.
Akitangaza matokeo ya kura za maoni, msimamizi wa uchaguzi jimbo la Vunjo, Elisa Mangure alisema, Grace alipata kura 80 kati ya 84 zilizopigwa sawa na asilimia 95 huku mgombea mwenza, Colin Msofe akipata kura 4 sawa na asilimia 4.76.
”Katika matokeo haya ya kura zilizopigwa na wajumbe wa mkutano mkuu wa chama, jimbo la Vunjo sasa namtangaza kuwa mshindi wa kura za maoni jimbo la Vunjo ni Grace Kiwelu aliyeshinda kwa ushindi wa kura 80 kati ya kura84 sawa na asilimia 95,” alisema
Grace pia katika kura nyingine za maoni zilizopigwa na wajumbe wa Baraza la Wanawake wa Chadema (Bawacha) kugombea ubunge wa viti maalum katika jimbo hilo.
Katika viti maalum, Grace aliibuka na ushindi wa kura za maoni 25 sawa na asilimia 83 huku mgombea mwenza Aziza Mohammed akiibuka na kura tano sawa na asilimia 16.
Grace amekuwa mbunge wa viti maalum tangu mwaka 2010.
Baada ya kuhitimishwa kwa kura hizo za maoni, kitakachofuatwa ni kamati kuu kupendekeza jina moja kati ya hayo mawili ya atakayepewa fursa ya kugombea kwenye uchaguzi mkuu.
Endelea kufuatilia MwanaHALISI Online na MwanaHALISI TV kwa habari mbalimbali
Leave a comment