ZAIDI ya watu 120 wamepoteza maisha huku kadhaa wakipotea kusikojuliakana kutokana na kimbunga kilichotokea katika nchi ya Msumbiji na Zimbabwe. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Kimbunga hicho kinachofahamika kwa jina la Ida, kilianzia nchini Msumbiji usiku wa Alhamisi tarehe 14 Machi 2019 na kusababisha vifo vya watu 62 na baadaye kiliingia nchini Zimbabwe na kuuwa watu 65.
Rais wa Zimbabwe, Emmerson Mnangagwa amekatisha ziara yake huku Abu Dhabi kutokana na kimbunga hicho cha Ida.
Waziri wa Mazingira nchini Msumbiji, Celso Correia amesema kimbunga hicho ni janga kubwa kuwahi kushuhudiwa nchini humo.
Mbunge wa Chimanimani nchini Zimbabwe, Joshua Sacco amesema watu kati ya 150 hadi 200 wamepotea kusikojulikana na kwamba vikosi vya ukoaji vinaendelea na shughuli za kuokoa wahanga.
Jana Jumapili wanajeshi walisaidia shughuli za uokoaji na kufanikiwa kuwaokoa wanafunzi 200 walimu na watumishi kadhaa waliokwama katika shule moja iliyoko Chimanimani.
Umoja wa Mataifa nchini Zimbabwe umesema kimbunga cha Ida kimeatihiri watu takribani 10,000.
Hii ni mara ya pili kwa Zimbabwe kukumbwa na janga hilo, ambapo mwezi Februari mwaka huu watu takribani 40 walifunikwa na vifusi katiika migodi nchini humo.
Leave a comment