Saturday , 20 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Fredrick Sumaye: Nimepozwa na uenyekiti wa Mbowe
Habari za SiasaTangulizi

Fredrick Sumaye: Nimepozwa na uenyekiti wa Mbowe

Spread the love
FREDRICK Tluway Sumaye, ameshindwa katika uchaguzi wa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Kanda ya Pwani, kufuatia kupigiwa kura nyingi za  Hapana. Anaripoti Hamis Mguta, Kibaha … (endelea).

Taarifa kutoka mjini Kibaha ambako mkutano huo wa uchaguzi umefanyika zinasema, kushindwa kwa Sumaye, kumetokana na hatua yake ya kuamua kugombea nafasi ya mwenyekiti wa taifa wa chama hicho.

Kwa mujibu wa mashuhuda wa uchaguzi huo, wapambe wa mwenyekiti wa sasa, Freeman Mbowe, wakiongozwa na Meya wa Ubungo, Boniface Jacob Mwangombola, walifika Kibaha na kuwaficha hotelini kwa lengo la kushawishi wasimpigie kura Sumaye.

Alisema, “tumefika hapa Kibaha kwa kazi moja tu. Kumzuia  Sumaye kuwa mwenyekiti wa Kanda ya Pwani, kwa kuwa ameamua kugombea nafasi ya Mbowe,” ameeleza mmoja wa viongozi wa Chadema anayemuunga mkono mwenyekiti wa chama hicho.

Alisema, “Sumaye anaadhibiwa kwa sababu hiyo ya uenyekiti wa taifa. Tulielekezwa kufanya hivyo, ili kumvunja miguu katika mbio zake hizo.” 

Kwa upande wake, Sumaye alisema, nilifahamu hili mapema, ingawa sikuwa nimeamini. Niliambiwa ndani ya chama chetu hakuna demokrasia. Kwamba, ukigusa uenyekiti wa Mbowe, basi utashughulikiwa. Mimi nimeamua kugombea na niko tayari kuadhibiwa kwa kutumia haki yangu hiyo ya Kikatiba.” 

“Kama kuchukua fomu ya uenyekiti wa taifa, ndio niadhibiwe. Niko tayari kwa hilo,” alieza Sumaye kabla ya mkutano huo kuanza.

Sumaye aliwaambia wajumbe wa mkutano mkuu, ni kweli kwamba aliamua kuchukua fomu ya kugombea nafasi hiyo, lakini hajaijaza na hivyo anaweza kuirejesha au kuichana.

Aidha, MwanaHALISI lilipata nafasi ya kuzungumza na mwanasiasa huyo shupavu nchini mara baada ya kumalizika kwa uchaguzi huo na kusema:

“Nilikuwa mgombea pekee wa kiti cha Kanda ya Pwani na sikutegemea kwamba ningeweza kushindwa. Ingawaje baada ya gazeti moja kutoa taarifa kwamba nimechukua fomu ya kugombea uenyekiti mambo yaliweza kubadilika, matokeo yaliyotokea ni kwamba nimeadhibiwa kwa kuchukua fomu ya kugombea nafasi hiyo,” amesema.

Sumaye alisema, “lengo langu lilikuwa ni kuonyesha ulimwengu kwamba Chadema huwa inatuhumiwa kwamba hakuna demokrasia na kwamba nafasi ya mwenyekiti haiguswi. Hivyo nilitaka kuvunja hiyo watu wajue kuna demokrasia na kwamba nafasi ya mwenyekiti ipo huru kwa mtu yoyote. Lakini kwa bahati mbaya kwa haya yaliyotokea, ni kinyume chake.” 

Katika uchaguzi huo inadaiwa kuwepo kundi kubwa pa wapambe wa Mbowe ambao walifika katika hoteli ya Njuweni mjini Kibaha, kwa lengo la kuhamasisha wapigakura kutomchagua Sumaye.

“Tumefika hapa kwa kazi moja tu. Nayo ni kumzuia Sumaye kuwa mwenyekiti wa Kanda kwa kuwa ameamua kutaka nafasi ya Mbowe,” ameeleza mmoja wa viongozi wa Chadema anayemuunga mkono mwenyekiti wa chama hicho.

Alipoulizwa mbunge wa Ubungo, Saed Kubenea juu ya kilichotokea kwenye uchaguzi huo, naye alisema, “hili jambo limepangwa. Ni kama ilivyokuwa kwa Yesu alipopelekwa kwa Pilato kwa ajili ya kusulubiwa.”

Anasema, kilichofanyika jana, ni watu kumchagua Baraba badala ya Yesu. Kwamba Pilato aliwauliza baada ya kuona huyu mtu (Yesu) hana hatia. Badala ya mwizi na jambazi Baraba. 

Alisema, “unajua Yesu aliletwa mbele ya Pilato kutokana na wivu viongozi wa Wayahudi. Basi Makuhani na wazee wakawashawishi umati wa watu kwamba waombe Baraba afunguliwe na Yesu auawe. Pilato akawauliza kwa mara ya pili, ni yupi mnataka niwafungulie?” 

Anasema, “…wakajibu, Baraba! Akauliza, sasa nifanye nini na huyu Yesu aitwaye Kristo? Wote wakajibu, asulubiwe! Akasema, kwa nini? Amefanya kosa gani? Lakini wao wakazidi kupiga kelele, asulubiwe.”

Akisoma matokeo ya uchaguzi huo, leo tarehe 28 Novemba 2019, Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa chama hicho (BAVICHA), Patrick ole Sosopi alisema, pamoja na mgombea wa nafasi hiyo kuwa mmoja, lakini alipaswa kushinda kwa zaidi ya asilimia 50 ya kura zote.

Alisema, “mheshimiwa Fredrick Sumaye, ameshindwa kutimiza takwa hili la kikatiba. Hivyo basi, nafasi hii, itagombewa tena baada ya kutangazwa na mamkala inayohusika.

Amesema, “kutokana na mgombea huyo kuwa mmoja, tulipiga kura za Ndio na Hapana. Matokeo ya kura hizo, kura za Ndio ziko 28 sawa na asilimia 36.3; moja imeharibika na kura za Hapana ziko 48, sawa na asilimia 62.3. Kutokana na matokeo hayo, nafasi hiyo itabaki kuwa wazi, mpaka mamlaka husika itakapoitangaza upya.”

Wakati uchaguzi ukienda hivyo kwenye nafasi ya mwenyekiti, katika nafasi ya Mhazini, Sosopi alisema, wagombea walikuwa wanne na wapigakura walikuwa 77 (Sabini na Saba).

Aliwataja waliogombea nafasi hiyo, kuwa ni Omari Juma Mkama ambaye alipata kura Sita, sawa na asilimia 7.8; Joseph James Dhahabu aliyepata kura Nane, sawa na asilimia 10.4; Florencia Taslima aliyepata kura 23 sawa na asilimia 29.9 na Michael Mtali, ambaye alipata kura 40 sawa na 51.9.

Kwa matokeo hayo, Sosopi alimtangaza Michael Mtali, kuwa mshindi wa uchaguzi huo. Mtali amewahi kushika nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya chama hicho, katika wilaya ya Kibaha.

Katika ngazi ya Makamu Mwenyekiti wa Kanda, Baraka Mwago, mwenyekiti wa chama hicho mkoa wa Pwani, aliibuka mshindi. Alichuana na Ruth Mollel, mbunge wa Viti Maalum; Isaya Mwita, Meya wa Halmashauri ya Jiji na Waziri Juma Mwenevale.

Hata hivyo, Mwago alilazimika kuingia kwenye duru la pili la kinyang’anyiro hicho, baada ya mshindi kushindwa kupatikana kwenye hatua ya kwanza. Katiba ya Chadema inasema, mgombea sharti atomize asilimia 50 ya kura. 

Matokeo ya uchaguzi huo kwenye duru la kwanza yalikuwa ni kama ifuatavyo: Waziri Juma Mwenevare, alipata kura Sita (sawa na asilimia 7.7), Mama Mollel alipata kura 13 (sawa na asimilia 16.8), Isaya alipata kura 28 (sawa na asilimia 36.3) na Mwago alipata kura 30 (sawa na asilimia 38.9).

Akizungumza matokeo ya uchaguzi huo wa makamu mwenyekiti, Sosopi alisema, “…tunalaziika kurudia uchaguzi kwa kuwashindanisha Isaya Mwita na Mwago.”

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

Dk. Mwakyembe : Zanzibar waliongoza kutaka Serikali 2 za muungano

Spread the love  MWANASIASA mkongwe nchini, Dk. Harrison Mwakyembe, amesema mjadala wa...

Habari za SiasaTangulizi

Rais Samia ataja mikakati ya kufikia trilioni 2 biashara Uturuki, Tz

Spread the loveWakati Tanzania na Uturuki zikidhamiria kuongeza kiwango cha biashara hadi...

BiasharaHabari za Siasa

Mavunde aagiza Perseus kuharakisha fidia Sengerema

Spread the loveWaziri wa Madini, Anthony Mavunde ameipongeza Kampuni ya Perseus kwa...

Habari za Siasa

Kigogo Chadema awanyooshea vidole vigogo serikalini kuhusu ripoti ya CAG

Spread the love  MWANACHAMA wa Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Boniface Jacob, amedai...

error: Content is protected !!