VIJANA kwa wazee mkoani Arusha leo tarehe 9 Machi 2019 wamejitokeza kumpokea Edward Lowassa, aliyekuwa mgombea urais kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema). Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Lowassa ambaye alirejea katika Chama Cha Mapinduzi (CCM) tarehe 1 Machi 2019, amepokewa kwa mara ya kwanza Arusha akiwa mwanachama wa CCM baada ya kuhama chama hicho Julai 2015.
Mgombea urais huyo wa Chadema na Waziri Mkuu aliyejiuzulu aliwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kisongo saa 6:20 mchana na kupokewa na viongozi mbalimbali wa CCM.
Miongoni mwa wanaCCM waliompokea ni pamoja na Daniel Awakii, Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM, Wilaya ya Karatu ambapo
Katika safari yake hiyo, Lowassa ameongozana na mke wake, Regina Lowassa, mtoto wake Robert na baadhi ya marafiki zake akiwemo Maxon Chizii, aliyekuwa Katibu wa CCM Wilaya ya Babati, Edward Porokwa na Hamisi Mgeja.
Baada ya mapokezi hayo, Lowassa ameelekea Monduli ambapo atapokewa na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Humphrey Polepole, viongozi na wanachama wengine.
Awali, Fred Lowassa, mtoto wa Lowassa alisema, familia yao yote imerejea CCM ili kumuunga mkono baba yake (Lowassa) na kwamba, wanajisikia faraja ‘kurudi nyumbani’.
“Baada ya mzee kurudi nyumbani CCM na sisi wote tumemuunga mkono kwa kurejea naye,” amesema Fred ambaye naye alihamia Chadema baada ya baba yake (Lowassa) kujiunga na chama hicho.
Lowassa alirejea CCM tarehe 1 Machi 2019 na kupokewa na Mwenyekiti wa chama hicho Rais John Magufuli, Makamu Mwenyekiti, Philip Mangula, Katibu Mkuu, Dk. Bashiru Ally na viongozi na wanachama wengine katika Ofisi ndogo wa CCM, Lumumba jijini Dar es Salaam.
Leave a comment