TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) nchini Tanzania imehamia rasmi katika ofisi zake mpya zilizopo Njedengwa jijini Dodoma. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea)
Kuhamia huko kwa NEC kutoka Dar es Salaam, kuna maanisha shughuli zote za Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020 zitafanyikia Dodoma ikiwemo uchukuaji na urejeshaji wa fomu za urais na utangazaji wa matokeo yake.
Hii ni mara ya kwanza tangu kuanzishwa kwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi takribani miaka 27 sasa kuwa na jengo lake yenyewe ambapo kwa muda mrefu Tume imekuwa na kilio cha kuomba kupatiwa ofisi moja ambayo ingetumiwa na wafanyakazi wote na hivyo kuokoa muda na gharama.
Tangu ilipoanzishwa tarehe 13 Januari, mwaka 1993 Tume ya Taifa ya Uchaguzi imekuwa ikifanya shughuli zake katika ofisi tatu tofauti jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na kundi la kwanza la watumishi walioripoti katika ofisi hizo jijini Dodoma leo Jumanne tarehe 14 Julai 2020, Mkurugenzi wa Uchaguzi, Dk. Wilson Mahera Charles amesema, hatua ya NEC kupata ofisi yake itaongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yake kwa kuokoa fedha na muda uliokuwa unatumika kutoka ofisi moja hadi nyingine.
Dk. Mahera ambaye amewapongeza watumishi waliojitolea kutangulia jijini Dodoma kwa ajili ya kuanza kazi katika ofisi hizo mpya ametaka watendaji wa Tume kujituma zaidi ili kazi zao ziakisi muonekano wa ofisi hiyo mpya.
Mkurugenzi huyo amesema, shuguli za Uchaguzi Mkuu wa Oktoba ikiwa ni pamoja na utoaji wa fomu za uteuzi kwa wagombea wa urais katika uchaguzi huo sasa rasmi zitafanyika katika jengo hilo jipya lililopewa jina la UCHAGUZI HOUSE lililopo eneo la Njedengwa nje kidogo ya jiji la Dodoma.
Leave a comment