KAMATI iliyoundwa na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa ajili ya kupitia mikataba ya wadau wa filamu, imetoa matokeo chanya kwa familia ya Marehemu Steven Kanumba na Amri Athumani (Mzee Majuto). Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Akizungumza bungeni jijini Dodoma leo tarehe 18 Aprili 2019, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Harrison Mwakyembe amesema, kazi ya kamati hiyo imepelekea familia ya marehemu Kanumba na Mzee Majuto kupatiwa mamilioni ya fedha kupitia kazi zilizofanywa na wasanii hao.
Akichanganua malipo hayo, Dk. Mwakyembe amesema, msimamizi wa mirathi ya marehemu Mzee Majuto aliingiziwa kiasi cha Sh. 30 milioni katika akaunti yake ya benki na Kampuni ya Ivory, Iringa pamoja na Pan Afrika Enterprises, ikiwa ni malipo ya ziada ya kazi za matangazo aliyofanya msanii huyo na kampuni hizo, enzi za uhai wake.
Aidha, Dk. Mwakyembe amesema Kampuni ya Tanform ya Arusha inatarajia kumkabidhi msimamaizi wa mirathi ya Marehemu Mzee Majuto kiasi cha Sh. 15 milioni, huku kampuni ya Azam-SSB ikiandaa malipo ya ziada ya sh. 20 milioni kwa ajili ya kumlipa msimamizi huyo.
Kwa upande wa marehemu Kanumba, Dk. Mwakyembe amesema msimamizi wa mirathi yake ambaye ni mama yake Flora Mtegoa, amekabidhiwa kiasi cha Sh. 15 milioni kama fedha za ziada kutokana na kazi alizofanya msanii huyo enzi za uhai wake.
Dk. Mwakyembe amesema, kampuni hizo zimelipa fedha hizo baada ya kamati iliyoundwa kwa ajili ya kupitia mikataba ya wasanii, kubaini kwamba kuna baadhi ya kampuni ziliingia mikataba mbovu na kwamba, ziliwalipa wasanii hao malipo madogo na kuathiri vipato vyao.
Leave a comment