TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) nchini Tanzania, imeongeza viwango vya faini kwa wagombea watakaofanya makosa ya kimaadili, katika kampeni na Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Dk. Wilson Mahera, Mkurugenzi wa NEC, jana Jumatano tarehe 27 Mei 2020 jijini Dar es Salaam alibainisha viwango hivyo wakati akizungumzia mabadiliko katika rasimu ya muongozo wa maadili, katika kampeni na uchaguzi huo.
Dk. Mahera alisema, faini kwa wagombea udiwani watakaofanya makosa, imeongezeka kutoka Sh. 100,000 hadi isiyozidi 150,000, wakati kwa wagombea ubunge ikiongezeka kutoka Sh. 500, 000 hadi isiyozidi 750,000.
Faini ya wagombea urais ikipanda kutoka Sh. 1,000,000, hadi isiyozidi 1,500,000.
“Viwango vya fedha vya faini kwa mtu anayefanya makosa vimeongezeka, kama mtu atafanya makosa kwenye ngazi ya udiwani, ilikuwa Sh. 100,000 lakini ilionekana kiwango kidogo, sasa tumeongeza itakuwa isiozidi Sh. 150,000,” alisema Dk. Mahera
“Kwa wabunge ilikuwa Sh. 500,000 lakini tumeongeza isiozidi Sh. 750,000, na kwenye urais ilikwua Sh. 1,000,000, tumeongeza isiozidi Sh. 1,500,000.”
Dk. Mahera alisema mabadiliko mengine yaliyofanyika katika rasimu hiyo, ni uainishaji wa wadau katika muongozo huo.
“Mabadiliko hayo yamelenga kuhakikisha maadili ni shirikishi na yanakuwepo kwa ajili ya kuhakikisha yanaleta uwazi katika utekelezaji, mojawapo ya changamoto ndogo iliyojitokeza, ilitakiwa tutaje wadau. Ambao katika rasimu hii tumewataja, Serikali, vyama vya siasa na NEC, na mambo mengine,” alisema Dk. Mahera.
Jaji Semistocles Kaijage, Mwenyekiti wa NEC, alisema mabadiliko hayo yamefanyika baada ya tume hiyo kupokea maoni kutoka kwa wadau wa uchaguzi, juu ya uboreshaji wa kanuni na miongozo ya itakayotumika kwenye uchaguzi huo.
“Kila mdau amepewa muda wa kutosha kuwaislisha maoni yao na mapendekezo ambayo tume iliyapitia na kuzingatia katika rasimu hiyo,” amesema Jaji Kaijage.
Leave a comment