Kabendera anayekabiliwa na mashitaka matatu, ikiwamo ukwepaji kodi ya Sh. 173 milioni; utakatishaji fedha na madai ya kujihusisha na magenge ya uhalifu, anazuiliwa katika gereza kuu la mahabusu, Segerea jijiji Dar es Salaam.
Akiwasilisha maombi ya kutaka Kabendera ashiriki ibada ya kuaga mwili wa mama yake, wakili wa mshitakiwa huyo, Jebra Kambole, aliimbia mahakama kuwa muhimu mteja wake, akaruhusiwa kushiriki msiba huo ambao ni muhimu kwake.
Alisema, “…tunaiomba mahakama imruhusu Kabendera akatoe heshima za mwisho kwenye mwili wa mama yake mzazi. Hili ni takwa la kisheria na Jamhuri (upande wa mashitaka), haitaathirika kwa lolote kwa mahakama kutoa ruhusa ya aina hiyo.”
Akaongeza: “mshitakiwa mwenyewe atakuwa chini ya ulinzi, na ibada itakuwa mchana kanisani; na kwamba kunakofanyika ibada ya mazishi huko Temeke siyo mbali na gerezani anakohifadhiwa Kabendera.”
Mama mzazi wa Kabendera, alifariki dunia juzi tarehe 31 Desemba 2019, katika hospitali ya Amana, jijini Dar es Salaam. Mwili wake unatarajiwa kusafirishwa kesho Ijumaa, kupelekwa kijijini kwao, Bukoba, mkoani Kagera.
Mwalimu Mujwahuzi amekutwa na mauti, siku chache baada ya kumuomba Rais John Magufuli, kumuachia huru mtoto wake huyo kwa maelezo kuwa anamtegemea kwenye maisha yake.
Mujwahuzi alisema, “namuomba rais Magufuli kuzingatia kuwa kwa umri wangu, namhitaji sana mwanangu Erick ambaye ni tegemeo langu pekee la matibabu.”
Mwandishi huyo wa habari alisababisha mamia ya watu waliokuwapo mahakamani, kujawa na huzuni, baada ya kumwaga chozi mbele ya halaiki.
Akisoma maamuzi ya mahakama hiyo, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu, Janeth Mtenga, ameeleza kuwa mahakama yake, haiwezi kutoa ruhusa ya aina hiyo, kwa kuwa ni kinyume cha sheria.
Kabla ya maamuzi hayo, upande wa Jamhuri, ulipinga maombi hayo kwa maelezo kuwa “mahakama haina mamlaka hayo.”
“Hata sisi tuna masikitiko makubwa na tunampa pole nyingi Kabendera kwa kufiwa na mama yake mzazi. Lakini maombi haya yapo mahakamani kinyume na sheria na hayawezi kutekelezeka,” ameeleza Wankyo Simon, wakili mkuu wa serikali.
Akizungumza nje ya mahakama hiyo, mara baada ya uamuzi huo, wakili Jebra amesema, uamuzi huu, hatukubaliani nao. Unakiuka misingi ya haki za binadamu. Tutaupinga.”
Leave a comment