TULIA Ackson, Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amemtaka Rashidi Shangazi, Mbunge wa Mlalo, mkoani Tanga kufuta kauli yake juu ya Kambi rasmi ya Upinzani Bungeni, baada ya kuiita kambi hiyo kuwa ni kambi rasmi ya upotoshaji, anaandika Hellen Sisya.
Tukio hilo limetokea leo bungeni mjini Dodoma katika kikao cha mwisho cha bunge ambapo mbunge huyo alikuwa akichangia mjadala unaohusu miswada mitatu ya ulinzi wa rasilimali na maliasili za nchi.
Kauli ya Mbunge huyo ilimnyanyua kitini Abdallah Mtolea, Mbunge wa Temeke (CUF) ambaye aliomba utaratibu kwa mujibu wa kanuni za bunge akitaka Shangazi afute maneno yake kwani ni kinyume cha kanuni hizo.
Naibu Spika alikubaliana na hoja ya Mtolea na kumtaka mbunge huyo kuheshimu kanuni za bunge na kuondoa maneno ya kuudhi aliyoyasema na badala yake kutumia maneno sahihi yanayotakiwa.
“Mheshimiwa Rashid Shangazi, naomba ufute maneno uliyoyasema kwasababu ni kinyume cha kanuni za bunge. Weka maneno yanayotakiwa kuwepo,” alisema Dk. Tulia.
Agizo hilo lilitekelezwa na Mbunge huyo.
Leave a comment