MBUNGE wa Mbeya Mjini, Dk. Ackson Tulia ameamua kutumia sehemu ya jengo la Mkuu wa Wilaya ya Mbeya kufanya majukumu yake ya kibunge badala ya ofisi ya mbunge. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mbeya…(endelea).
Akieleza sababu za kukwepa ofisi iliyokuwa ikitumiwa na Joseph Mbilinyi maarufu Sugu (Chadema), aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Dk. Tulia amesema ‘nimekwepa mlolongo wa kukabidhiana ofisi.’
“Ningesema nisubiri makabidhiano ya ofisi, nitavuta muda mwingi kama mnavyojua,” amesema Dk. Tulia muda mfupi baada ya kukutana na wananchi na kusikiliza kero zao.
Dk. Tulia ambaye ni Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri, alitangazwa kumshinda Sugu, hata hivyo ushindi wake umeingia ukakasi baada ya Sugu na vyama vya upinzani nchini kukosoa mchakato mzima wa uchaguzi mkuu kwamba, uligubikwa na hila.
Miongoni mwa vipaumbele vya Dk. Tulia kwa wakazi wa jimbo lake ni pamoja na kujenga kiwanda cha taulo za kike, kuimarisha huduma za za afya, kuboresha miundombinu ya elimu, kuboresha soko la wafanyabishara wadogo kwenye eneo la uwanja wa ndege wa zamani.
Leave a comment