MBUNGE wa Buchosha, Dk. Charles Tizeba aliyekuwa Waziri wa Kilimo ameibua shangwe bungeni kwa kushangiliwa na wabunge aliposimama kwa ajili ya kuuliza swali la nyongeza. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Dk. Tizeba aliyevuliwa wadhifa wa uwaziri wa kilimo na Rais John Magufuli tarehe 10 Novemba 2018 na nafasi yake kuchukuliwa na Japhet Hasunga, kwa mara ya kwanza leo tarehe 13 Novemba 2018 alisimama bungeni kama mbunge wa kawaida.
Aliposimama kwa ajili ya kuuliza swali, alianza kwa kumshukuru Rais Magufuli kwa fursa aliyompa ya kuwa waziri pamoja na kuushukuru uongozi wa bunge kwa ushirikiano alioupata wakati akiwa kwenye wadhifa huo, ndipo wabunge walizidisha kumshangilia kwa kupiga makofi.
Katika swali lake la nyongeza, Dk. Tizeba alihoji kama serikali inaendelea na dhamira yake ya kujenga vivuko vipya kutokana na jimbo lake lenye visiwa takribani 28 kuwa na uhaba wa vivuko, kitendo iinachohjatarisha usalama wa wananchi wa jimbo hilo.
“Jimbo langu la Buchosa linavyo visiwa zaidi ya 28 kuna vivuko viwili, kimoja kimepitwa na wakati kinakuwa ‘overloaded’ kinaelemewa na mizigo, wakati mwingine watu wanaogopa kupanda, je comitment (dhamira) ya kujenga kivuko kipya iko pale pale au lah,” amehoji Dk. Tizeba.
Akijibu swali hilo,Naibu Waziri Ujenzi na Uchukuzi, Mhandisi Elias Kuandikwa amesema utaratibu wa kuboresha usafiri katika jimbo hilo unaendelea na kwamba serikali imeunda timu ya kutembelea vivuko vilivyopo, kisha kurekebisha kivuko kilichoharibika .
Leave a comment