RAIS wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein amesema, anaondoka madarakani huku akifanikiwa kuacha visiwa hivyo (Unguja na Pemba) vikiwa na amani. Anaandika Mwandishi Wetu, Zanzibar…(endelea).
Akizungumza wakati wa kuaga watumishi wa serikali aliyokua akiongoza tangu mwaka 2010, amewataka kuendelea kukichagua Chama Cha Mapinduzi (CCM) ili kuendeleza amani hiyo.
“Naondoka madarakani nikiiacha nchi yenye amani. Ninaondoka madarakani huku nikiwa nimeacha milango yangu ya ushauri wazi kwa anayetaka kuja, lakini ajitahadhari sitaki majungu na fitina,” amesema Dk. Shein.
Amesema, katika maisha yake ametumikia Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa miaka 51 na kwamba, katika utawala wake Zanzibar, amefanikiwa kujenga misingi mizuri ya uongozi, utawala bora, maendeleo.
“Namaliza muda wa utumishi wangu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Muungano kwa muda wa miaka 51, nikiwa nimefanikiwa kujenga misingi mizuri ya utawala bora, naondoka nikiacha amani na utulivu vimetawala.
“Ninaondoka madarakani huku nikiwa nimepata mafanikio makubwa katika utendaji wa utumishi wa serikali ikiwamo kufanya marekebisho ya sheria katika Baraza la Wawakilishi zipatazo 128,” amesema.
Pia amempongeza Rais John Magufuli kwa kufanyakazi naye kazi kwa ushirikiano na kuwa, (Rais Magufuli) ni kiongozi mwenye uwezo mkubwa wa kubuni mambo yenye maslahi makubwa kwa Taifa.
Leave a comment