HALI ya mambo ndani ya Wizara ya Maliasili na Utalii siyo shwari na sasa Waziri wa wizara hiyo, Dk. Hamisi Kigwangalla amelazimika kumsimamisha kazi Mkurugenzi wa Wanyama Pori kutokana na tuhuma mbalimbali.
Dk. Kigwangalla amemuagiza Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Maj. Gen. Gaudence Milanzi, kumsimamisha kazi Mkurugenzi wa Wanyama Pori, Profesa. Alexander Songorwa mara moja.
Ametoa agizo hilo akiwa ndani ya Hifadhi ya Serengeti, ambapo amefanya ziara ya kushtukiza na kuuzunguka mpaka wote wa mashariki wa eneo hilo ambalo linapakana Pori Tengefu la Loliondo ambalo lina mgogoro wa muda mrefu.
Waziri Kigwangalla amesema Mkurugenzi huyo amekuwa akifanya kazi kwa maelekezo ya mwekezaji wa Kampuni ya Utalii wa Uwindaji ya OBC (maarufu kama kampuni ya kiwindaji ya wafalme wa Dubai). Kampuni hii imekuwa ikihusishwa na kashfa kwa miaka zaidi ya 26.
Aidha Prof. Songorwa amekuwa akihusishwa na kashfa ya kushiriki kugawa vitalu vya uwindaji kinyume cha sheria.
Wiki mbili zilizopita Waziri Kigwangalla alisitisha mchakato wa kuhuisha leseni za uwindaji uliofanywa na Prof. Jumanne Maghembe, aliyekuwa mtangulizi wake katika wizara hiyo kutokana na madai ya kuwapo rushwa na kukosekana uwazi kwenye mchakato huo. Pia ameelekeza mchakato wa kugawa vitalu sasa ufanywe kwa njia ya mnada.
Pia, ameelekeza Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru)waanze kuchunguza kashfa za rushwa dhidi ya kampuni ya OBC na waanze kwa kumhoji Mkurugenzi wa OBC, Mollel ambaye amekuwa akijigamba kila kona kuwa alimhonga Maghembe dola 200,000, huyu kijana Kigwangalla dola 100,000 inamtosha! Dk. Kigwangalla amesisitiza hahongeki na ndiyo maana jitihada za kumuona zimekwama, na hata alipotumiwa ujumbe kupitia watu wake wa karibu alikataa.
Ili kuimarisha ulinzi wa mpaka wa Mashariki mwa Serengeti, Waziri Kigwangalla amewaondoa askari wote wa kituo cha geti la Kleins kwa kuwa wamekuwa wakitumika na mwekezaji huyo ambaye ana mahusiano ya karibu na Prof. Songorwa.
Leave a comment