DK. Bashiru Ally, Katibu Mkuu wa CCM amesema kitendo cha wabunge na madiwani wa vyama vya CUF na Chadema kujivua unachama na kujiunga na chama chake, ni faida kwa vyama hivyo vya upinzani. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea)
Dk. Bashiru ameyasema hayo leo tarehe 15 Agosti, 2018 wakati akihojiwa na kituo kimoja cha luninga kuhusu hasara iliyongia Taifa katika kuitisha uchaguzi mdogo kufuatia uamuzi wa wabunge hao kujivua ubunge.
Ameeleza kuwa, sababu zinazotolewa na wabunge hao pindi wanapohama ni ujumbe tosha kwa vyama vya upinzani wanakotoka, utakaowasaidia kujitathimini kama wako sahihi au la!.
“Ndiyo mfumo uliopo ni kwamba mtu akitoka kwenye chama baada ya kuridhika kwamba chama hakifai na hakifuati misingi niliyoifuata sina sababu ya kuwa mtumwa, na akiamua kuondoka utaratibu unasema amepoteza kila kitu…Ndiyo tiba ninayosema, kuna hasara ya kifedha lakini kuna faida ya kutibu majeraha kwenye mfumo wa kisiasa kwanza,” amesema Dk. Bashiru na kuongeza.
“Ni ishara ya kutuma ujumbe kwa vyama kwamba mkianza kubinafsisha vyama watu watawakimbia, badala ya kukaa na vyama vinavyowachonganisha vinavyoodhofisha mchakato wa kisiasa na mfumo wa kidemokrasia hiyo nayo gharama inaweza kuwa halali, gharama ya kujitathimini kama taifa na vyama vyenyewe kujitathimini pengine ingekuwa vigumu kwa vyama vyenyewe kujijua kama viko sahihi au haviko sahihi.”
Leave a comment