FIKRA kwamba, Rais John Magufuli anapaswa kuendelea kuwepo madarakani hata baada ya kumaliza muhula wake wa pili iwapo atachaguliwa, wametakiwa kuzika fikra hizo. Anaripoti Danson Kaijage…(endelea).
Dk. Bashiru Ally, Katibu Mkuu wa CCM amewataka makada wa chama hicho kutoomba dua hiyo na kuwa, ameshauri kuimarisha chama chao ili kiendelee kutoa viongozi bora.
Akizungumza katika Uzinduzi wa Mkakati Maalum wa CCM wa kukomaza demokrasia nchini uliofanyika jijini Dodoma, Dk. Bashiru amesema, chama hicho kina kazi ya kuhakikisha kinatoa viongozi bora kama Rais Magufuli, na si kubadili utaratibu na kuomba kiongozi huyo kuongoza muda mrefu.
Amesema, CCM ina mbegu za kuzalisha viongozi bora na kuwatoa wasiwasi baadhi ya watu wanaofikiria hatma ya Tanzania baada ya Rais Magufuli kumaliza uongozi wake.
“Naomba kuhitimisha mjadala usio rasmi, unaoendelea kuhusu hatma ya nchi hii baada ya Dk. John Pombe Magufuli. Hatma ya nchi hii iko mikononi mwa wana-CCM.
“CCM inahazina ya viongozi bora wakati wote wanaCCM na hasa wakina mama wana CCM wanambegu bora za kuzalisha viongozi wa kutosha,” amesema Dk. Bashiru na kuongeza;
“Kwa hiyo kazi ya kutuhakikishia kuwa na viongozi bora kama Dk. Magufuli si kuomba dua ya kukaa muda mrefu madarakani au kubadilisha taratibu tulizonazo, bali ni kuimarisha chama chetu, kwa hiyo mkakati huu unalenga kutukumbusha kwamba CCM ina hazina ya viongozi bora.”
Leave a comment