DAKTARI Bashiru Ally, Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM), amewatuhumu baadhi ya wateule wa Rais John Magufuli, kwamba hawana uaminifu, kitendo kinachopelekea wananchi kuhofia kuwapa taarifa za uhalifu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Morogoro … (endelea).
Akizungumza katika ziara yake mkoani Morogoro, Dk. Bashiru amedai kwamba, kuna baadhi ya wakuu wa mikoa na wilaya, huwataja kwa wahalifu, wananchi wanaowapa taarifa za uhalifu ikiwemo uhujumu uchumi. Badala ya kuzifanyia kazi taarifa hizo.
Dk. Bashiru ametoa madai hayo wakati akizungumzia tukio la mwananchi ambaye hakumtaja jina, aliyempa taarifa za wakwepa kodi, badala ya kuzifikisha taarifa hizo kwa mkuu wa wilaya au mkoa husika.
“Yuko mwananchi mmoja kanipa taarifa, kaja ofisini kanipigia simu Dar es Salaam, akasema katibu mkuu nina ushahidi wa watu wanaoihujumu serikali, twende nikuonyeshe wapi sukari ya magendo ipo. Wakwepa kodi wapo. nikatafuta watu,” ameeleza Dk. Bashiru na kuongeza:
“Baadae napigiwa simu imekamatwa sukari ya magendo. Mwananchi aliyetoa taarifa ni mnyonge kabisa na wala haihitaji malipo yoyote yale. Sasa kwa nini hakumuamini mkuu wa mkoa na anaye pale, mwenyekiti wa mkoa na anaye pale, mkuu wa wilaya na anaye pale. Akaja kwa Katibu Mkuu CCM?”
Dk. Bashiru amesema anasikitishwa na kitendo hicho cha wananchi wenye taarifa za uhalifu kukimbilia kutoa taarifa zao kwa viongozi wa ngazi za juu, badala ya kuzifikisha taarifa hizo kwa wakuu wa mikoa na wilaya.
“Kila ninapokwenda naacha simu yangu, na habari ninazokusanya zinakuwa na matokeo mazuri sana. Kinachosikitisha, wananchi wanaleta habari juu wakati chini kuna viongozi,” amesema Dk. Bashiru.
Katibu huyo wa CCM amewataka wakuu wa mikoa na wilaya, kujenga utaratibu wa kuaminiwa na wananchi, ili waweze kupatiwa taarifa za wahalifu ikiwemo wakwepa kodi na wahujumu uchumi.
Tujenge utaratibu wa kuaminiwa na wananchi, wanazo taarifa nyingi kuhusu masuala yanayoendelea. Wanawajua wezi na wahujumu lakini wanaogopa watakayempa taarifa, badala ya kufanyia kazi anamzunguka anamchoma.
Leave a comment