MAALIM Seif Sharif Hamad, Mwenyekiti wa Chama cha ACT-Wazalendo, yupo mdomoni mwa Dk. Bashiru Ally, Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Dk. Bashiru ametoa kauli hiyo leo tarehe 8 Julai 2020, wakati akihojiwa na Kituo cha Uhai TV.
Amesema, licha ya kwamba Maalim Seif anagombea urais kupitia ACT-Wazalendo, CCM haitishiki kwa kuwa kimemshinda mara zote alizogombea kuanzia uchaguzi mkuu wa mwaka 1995.
Maalim Seif amegombea urais mara tano visiwani humo (1995, 2000, 2005, 2010, 2015) kupitia Chama cha Wananchi (CUF). Mara zote hizo amekuwa akidai, anashinda lakini ushindi wake unaporwa na CCM.
Tayari Maalim Seif amechukua fomu ili kuomba ridhaa ya chama chake kuteuliwa kugombea urais visiwani humo kupitia ACT-Wazalendo.
Soma zaidi:-
Akizungumzia hatua hiyo ya Maalim Seif kugombea tena urais wa Zanzibar, Dk. Bashiru amesema, mwanasiasa huyo mkongwe hatoshinda katika uchaguzi huo.
Amesema, historia ya Maalim Seif yake ni kushindwa katika uchaguzi, hivyo na kuwa hilo haliwezi kubadilika kwenye uchaguzi wa mwaka huu akisisitiza, mwaka huu (Maalim Seif) anagombea kupitia chama kipya na kisicho na nguvu.
Dk. Bashiru amesema, sababu hizo zitaifanya CCM kushinda katika uchaguzi wa urais wa Zanzibar, unaotarajiwa kufanyika mwezi Oktoba 2020.
“Kwa upande wa Zanzibar, tutakua na mgombea mpya kabisa, lakini wenzetu wanaweza kusimamisha mgombea ambaye amekuwa akishindwa kila mwaka.
“Maalim Seif, yeye ni mzoefu wa kushindwa lakini zamu hii ni mgeni katika chama chake, kwa hiyo leo hii tunashindana na mzoefu wa kushindwa na mgeni katika chama ambacho hakina mtandao,” amesema Dk. Bashiru.
Leave a comment