DAKTARI Hassan Abbasi, Msemaji Mkuu wa Serikali ambaye pia ni Mkurugenzi wa Idara ya Habari, MAELEZO amewataka waandishi wa habari nchini kufanya kazi zao kwa uhuru, bila uoga kwani serikali ipo tayari kupokea maoni ya ukosoaji. Anaripoti Charles William … (endelea).
Dk. Abbasi amesema hayo hii leo jijini Dar es Salaam, katika sherehe za waandishi wa habari waliohitimu mafunzo chini ya ufadhili wa taasisi ya Tanzania Media Foundation (TMF), ambapo alikuwa mgeni rasmi.
“Wakati tunatengeneza Sheria ya Huduma za Habari, miongoni mwa vifungu nilivyopigania kiwepo kilikuwa ni kifungu cha 52 (2) kinachosema hakuna kosa kwa mtu anapokosoa serikali.
“Msiogope kukosoa, tuambieni tunakosea wapi, semeni tunakosea wapi labda kwenye sekta ya viwanda au kwingine na sisi tutafanyia kazi. Usitukane wala kukashifu mtu, usikosoe lakini kwa kusema uongo. Pia kuna mambo yanayohusu usalama wa Taifa lazima yazingatiwe.”
Dk. Abbasi ameipongeza TMF kwa kutoa mafunzo kwa waandishi ili waweze kubobea katika habari za uchunguzi za maendeleo pamoja na eneo la usalama wa barabarani, na kuwataka kutumia ujuzi waliopata kuisaidia serikali kwa kukosoa na kufichua mambo mbalimbali.
Fausta Musokwa, Kaimu Mkurugenzi wa TMF amesema taasisi hiyo itaendelea kutoa mafunzo na ruzuku kwa waandishi na vyombo vya habari ili waweze kuandika habari zitakazosaidia uwazi na uwajibikaji serikalini.
“Taasisi yetu ilianza mwaka 2008 kama mfuko wa wanahabari, mpaka sasa tumetoa mafunzo ya ubobezi (fellowship) kwa waandishi zaidi ya 120 na tutaendelea kufanya hivyo.”
Halima Shariff, mwenyekiti wa bodi ya wakurugenzi ya TMF amewataka waandishi kutochoka kufanya uchunguzi na kuibua mambo mbalimbali kwa maslahi ya nchi na wananchi pamoja na changamoto zinazowakabili.
Jumla ya waandishi 14 wamehitimu mafunzo yaliyokuwa yakiendeshwa na TMF kwa miezi sita kutoka Juni mpaka Januari mwaka 2018. Waandishi tisa wamehitimu mafunzo ya ubobezi ya kuandika habari za maendeleo na watano wamebobea katika uandishi wa habari za usalama barabarani.
Leave a comment