WIZARA ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi imeombwa kuangalia uwezekano wa kuipa usajili shule ya sekondari ya Matuli iliyopo wilayani Morogoro vijijini ili ianze kutumika, anaandika Christina Haule.
Hatua hiyo itawasidia wanafunzi wa eneo hilo wanaotembea kilimita 21 kwenda shule ya sekondari ya kata ya Ngerengerea.
Ombi hilo limetolewa leo na na Diwani wa Kata ya Matuli Tarafa ya Ngerengere katika Halmashauri ya Morogoro vijijini, Lukas Lemomo kwenye mkutano wa hadhara na wananchi wake kuzungumzia maendeleo ya elimu kwenye kata hiyo.
Diwani huyo amesema kuwa licha ya majengo ya shule hiyo kukamilika kwa ajili lakini imeshindwa kaunza kuchukua wanafunzi kutokana na kutokamilisha usajili.
Amesema kukosekana kwa usajili wa shule hiyo kumefanya wanafunzi kulazimika kusoma shule iliyopo kata nyingine ambayo ipo umbali mrefu.
“Tayari madarasa mawili ya kidato cha kwanza na cha pili tumeshayajenga kwa kushirikisha nguvu za wananchi kwa na katika kipindi cha miaka miwili tutakuwa tayari tumemalizia madarasa mengine mawili wakati watoto wanaendelea kusoma, Waziri Ndalichako tunaomba liangalie hili ” amesema
Aidha, amewaomba wananchi kutochoka kuendelea kuchangia na kujitolea katika kuhakikisha kata hiyo inapata shule ya kata ya sekondari na kwamba fedha zote zinazochangwa zipo salama katika akaunti ya kata na zitatumika kuendeleza ujenzi kama ilivyopangwa.
Leave a comment