MWANAMUZIKI wa kizazi kipya Nasibu Abdul maarufu kwa jina la Diamond Platnum leo tarehe 9 Agosti, 2018 amezua kizaazaa kwenye msiba wa Amri Athumani maarufu kwa jina la King Majuto. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Diamond alifika kwenye ukumbi wa Kareem Jee wakati ambao shughuli ya kuaga mwili wa King Majuto ikiendelea na kuzuiwa kutokana na kuchelewa kufika eneo la tukio.
Maofisa wa Usalama wa Rais walimzuia Diamond kutokana na kuchelewa kufika kwenye msiba huo baada ya Rais John Magufuli kuwasili.
Utaratibu wa serikali unaelekeza kwamba rais anapaswa kuwa mtu wa mwisho kuingia eneo la tukio na kuwa wa kwanza kutoka.
Kutokana na kuzuiwa, Diamond alilazimika kubaki nje ya ukumbi akisubiri mwili wa King Majuto utolewe nje tayari kwa safari ya kuelekea Tanga kwa ajili ya mazishi kesho Ijumaa.
Wakati mwili wa King Majuto ulipokuwa ukitolewa nje, Diamond alijiunga sawa na watu wengine katika kuupokea mwili huo lakini ghafla watu waliongezeka kwa mkupuo upande aliokuwepo Diamond.
Hatua hiyo ilisababisha msongamano kuelemea upande wa Diamond jambo lililowasukuma walinzi wake (Diamond) kumwondoa eneo hilo ili kutuliza vurugu zilizokuwa zimeanza kuibuka.
Hata hivyo, baada ya Diamond kundolewa eneo hilo na walinzi wake, idadi kubwa ya watu nayo ilimfuata nyuma na kulipa jeneza mgongo.
Walinzi wake wake walilazimika kuanza kuwasukuma watu waliokuwa nyuma ya Diamond na mbele yake ambao tayari walikuwa wamemzingira. Walinzo hao walimwelekeza moja kwa moja mpaka kwenye gari lake.
Baada ya Diamond kuingia kwenye gari lake, alifunga vioo na kutulia huku walinzi wake wakizungua nje ya gari hilo kwa ajili ya usalama.
Leave a comment