ASAJILE Mwambambale, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa na Mkuu wa Wilaya hiyo, Adam Mgoy nusura watumbuliwe. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Akizungumza kwenye uwekaji jiwe la msingi la ujenzi wa handaki kwenye njia ya reli ya treni ya kisasa (SGR), leo tarehe 29 Juni 2020 Kilosa mkoani Morogoro, Rais Magufuli amewataja wateule wake hao kwamba wanamakunyanzi kwenye utendaji wao.
Kiongozi huyo wa nchi amesema, wateule katika uongozi wake hawawezi kuwa na furaha kwa kuwa, hata yeye hana furaha kwani wanapaswa kuumiza na kero za wananchi.
Akizungumzia migogoro wilayani humo, Rais Magufuli amesema anazo taarifa kwa watendaji wake kutenda kinyume na taratibu za kazi zao zinavyowaelekea.
Miongoni mwa waliotajwa na Rais Magufuli kwenye hadhara hiyo ni pamoja na Mkurugenzi na Mkuu wa Wilaya ya Kilosa.
“Niwaambie katika kipindi changu hamtafurahi sana, hata mimi sipati raha. Ni lazima tuteseka kwa ajili ya kutatua kero za wananchi. Nimeambiwa Mkurugeni wa hapa ana matatizo, ajirekebishe.
“Siwezi nikamtumbua mbele ya askofu. Madhambi yake anayajua, ameuza eneo kule, kikao kikakaa siku hiyo hiyo na mkataba akasaini siku hiyo hiyo, kwa taarifa za pembeni zinasema aliingiziwa mil 400,” amesema Rais Magufuli.
Amesema, pia Mkuu wa Mkoa wa Kilosa naye ana taarifa zake kuhusu utendaji wake na migogoro wilayani mwake. Na kwamba, kama anaowateua hawawezi kazi, ni bora wakaacha kazi.
“Nawaomba viongozi badilikeni, mkiteuliwa mkiona hamuwezi achene kazi. DC wa Kilosa nawe jirekebishe. DC umeenda Kimamba ukaanza kuwazuia watu kwenye mashamba tena yanamilikiwa na wageni, badala ya kuwatetea watu wako, unawatetea ambao huji hata wamezaliwa kijiji gani,” amesema.
Kwenye hotiba yake, Rais Magufuli amesema kumekuwa na wageni wanaomiliki ardhi kinyume na sheria za nchi, ameagiza ardhi hiyo ipokwe na kisha igawiwe kwa wananchi ili wanufaike nayo.
Pia amewataka wakazi wa eneo hilo kulinda mradi huo wa reli na kwamba, ujenzi wa reli hiyo ya kisasa Dar hadi Moro umekamilika kwa asilimia 85 na Morogoro hadi Makutupora umejengwa kwa asilimia 30.
“Niliamua leo nitembee kwa miguu, ujenzi wa reli hii ambayo ghrama yake ni zaidi ya tril tatu, fedha zote hizi zimetolewa na Watanzania, hawa makandarasi mnaowaona kutoka Urusi, wameajiriwa kwa fedha za Watanzania,” amesema na kuongeza:
“…hii ndio inanifanya sisi Watanzania sio masikini, hapa hakuna fedha hata ya kukopa, ni keshi imetoka hapa. Ukitoa keshi hujidai? Ndio maana nawaomba Watanzania wenzangu tutembee kifua mbele.”
Leave a comment