MAMLAKA ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (Dawasa), imechukua miradi ya kijamii 22 iliyokua chini ya halmashauri ya Temeke na kuiendeleza ikiwa na lengo la kuboresha upatikanaji wa huduma hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Miradi hiyo ya kijamii, iliyochukuliwa iko maeneo ya; Kitunda, Juabile, Kipunguni, Jaika, Korongo Kivule, Juanya Kivule, Mzinga A, Mwanagati, Mzinga B na Matumbi.
Mingine ni; Keko bora, Keko Mwanga A, Keko Manga B, Machinjioni A, Mbagala Kuu, Kijichi, Serenge, Kingugi, Njia panda ya Mwinyi, Juhudi, kwa nyoka na Mlamayo.
Miradi hiyo kwa asilimia kubwa inatumia visima kama vyanzo vyake vya maji huku ikiwa na uwezo wa kuhudumia wakazi zaidi ya 4,000.
Mhandisi wa Dawasa Temeke, Mhandisi Ramadhani Sangali akizungumza na waandishi wa habari jana Jumatano tarehe 6 Januari 2021 alisema, miradi hiyo ilikua chini ya halmashauri na imekabidhiwa Dawasa mwanzoni mwa mwaka 2020 kwa usimamizi na uendeshaji.
Alisema, kwa kiasi kikubwa miradi hiyo ya kijamii imeisaidia kuongeza makusanyo kwa Mkoa wa kihuduma Dawasa Temeke, lakini pia, imeleta mabadilliko ya kiutendaji, kwani imeweza kuondoa malalamiko kutoka kwa wananchi ya ukosefu wa maji kwa kiasi kikubwa.
Kutokana na kugawanyika kwa Mkoa wa kihuduma Dawasa Temeke na kupatikana Mkoa wa kihuduma Dawasa Mbagala, miradi hiyo ya kijamii itagawanywa katika mikoa ya kihuduma Dawasa Temeke na Mbagala.
“Mamlaka ilichukua miradi hii ya kijamii kutoka halmashauri kwa lengo la kuweza kuisimamia na kufikisha huduma ya maji kwa wakazi wote wa maeneo husika, lakini pia lengo lingine likiwa kuweza kuboresha huduma za maji ambazo awali zilikua zikisuasua,” alisema Sangali.
Dawasa inaendelea kuboresha huduma ya maji safi kwa kuhakikisha inasimamia utoaji huduma kwa watumiaji maji ya visima binafsi na vya Jumuiya kwenye maeneo ambayo mtandao wa Maji kutoka Ruvu juu na Ruvu chini haujafika.
Leave a comment