ABUU Kimboko, Mkazi wa Mbagala Rangitatu, amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam kwa mashtaka mawili, likiwemo la kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya aina ya Heroin. Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam…(endelea).
Akisomewa mashtaka hayo na wakili wa serikali Elia Atanus, mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Salum Ally leo tarehe 14 Januari 202, Kimboko anadaiwa tarehe 29 Desemba 2019, katika maeneo ya Mbagala Zakhiem, alijihusisha na biashara ya dawa za kulevya aina ya Heroin yenye uzito wa gram 273.45.
Pili; anakabiliwa na shitaka la utakatishaji fedha, ambapo inadaiwa kati ya tarehe 1 – 29 Desemba 2019 alijipatia kiasi cha Sh. 990,000 huku akifahamu fedha hizo ni zao la biashara haramu ya dawa za kulevya.
Wakili Atanus amedai, upelelezi wa shauri hilo upo mbioni kukamilika. Mtuhumiwa hakutakiwa kujibu chochote kwasababu, mahakama hiyo haina uwezo wa kusikiliza kesi ya uhujumu uchumi. Kesi imeahirishwa hadi tarehe 28 Desemba 2020 ambapo itakuja kutajwa.
Leave a comment