CHAMA cha Wananchi (CUF) kimetoa msimamo wake kuhusu kuhama kwa waliokuwa viongozi, wabunge na madiwani wa chama hicho, kikisema kuwa kitafanya vikao vyake vya kitaifa hivi karibuni ili kujaza nafasi wazi za uongozi zilizokuwepo. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea).
Msimamo huo wa CUF umetolewa leo tarehe 19 Agosti, 2018 na Naibu Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano, Mbarala Maharagande, akisema kwamba chama hicho kitaitisha vikao vya Kamati ya Utendaji ya Taifa na Baraza Kuu la Uongozi la Taifa ili kufanya tathmini ya pamoja na kuweka mikakati thabiti ya kuendeleza mapambano ya kisiasa, kukilinda Chama na kujaza nafasi wazi za Uongozi zilizokuwepo.
Julius Mtatiro aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi ya CUF Taifa ni miongoni mwa watu waliohama chama na kujiuzulu vyeo vyao, wengine ni Maulid Mtulia aliyekuwa Mbunge wa Kinondoni, na Mussa Kafana aliyekuwa Naibu Meya wa Jiji la Dar es Salaam.
Kuhusu kauli ya CUF juu ya wabunge, madiwani na viongozi wake waliohama, Maharagande amesaema chama hicho hakina pingamizi kwa kiongozi au mwanachama yeyote pale atakapoona ameshindwa kusimamia malengo na madhumuni ya chama hicho, kujiondoa ndani ya chama.
Hata hivyo, Maharagande amesema hoja zilizowapelekea kuhama hazina mashiko na kwamba wametanguliza masilahi yao binafsi. Na hivyo kitendo hicho kinawapa fursa nzuri ya kujipanga upya kwa kuwa na wapambanaji sahihi kwenye nafasi husika.
“Kumezuka taharuki kwa wanachama wetu na Watanzania wapenda Mabadiliko nchini kufuatia baadhi ya Viongozi wa Chama kwa nafasi za Kiserikali, madiwani na Wabunge kujiuzulu nafasi zao na kujiunga na CCM.
Hakuna sababu ya kutaharuki zaidi ni kuwaonea huruma kwa sababu wamekubali kujivunjia heshima zao mbele ya jamii iliyowaamini na kuwa watumwa wa kifikra,” amesema Maharagande.
Leave a comment