NAIBU Spika wa Bunge la Jamhuri, Dk. Tulia Akson, amelitangazia Bunge kuwa mmoja wa wabunge wa Bunge hilo, amepatwa na virusi vya Corona. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Akizungumza bungeni mchana huu, muda mfupi kabla ya kughairisha Bunge, Dk. Tulia alisema, mbunge huyo alithibitika kuwa na ugonjwa huo, mwishoni mwa wiki iliyopita.
Naibu Spika Tulia, hakutaja jina la mbunge ambaye amesema ameambukizwa virusi hivyo.
Hata hivyo, baadhi ya wabunge wamemwambia mwandishi wa habari hizi kuwa mbunge huyo anatokea moja ya majimbo ya mkoa wa Dar es Salaam.
Alisema, “tumepata taarifa kuwa mbunge mwenzetu alikuja Dodoma kutokea Dar es Salaam, Jumatano iliyopita. Akiwa hapa Dodoma akaanza kujisikia vibaya na hivyo akalazimika kurudi Dar es Salaam
“Alipofika Dar es Salaam akaenda hospitali ambako baada ya kufanyiwa uchunguzi na madaktari bingwa wanaojihusisha na ugonjwa huu, amethibitika kuwa na maambukizi.”
Dk. Tulia alitoa tangazo hilo, wakati akighairisha Bunge kupisha msiba wa mbunge wa Viti Maalum (CCM), Gerturde Pangalile Rwakatare.
Mbunge Rwakatare ambaye ni Askofu wa Kanisa la Assembliess of God – maarufu kama Mlima wa Moto – alikutwa na mauti asubuhi ya kuamkia leo Jumatatu.
Leave a comment