SERIKALI ya China imepanga kutoa Yuan RMB 300 Milioni (Tsh. 98,084,910,435.8), kwa ajili ya kuimarisha ulinzi nchini ikiwemo, ujenzi wa Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa, jijini Dodoma. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Hayo amesema Jenerali Venance Mabeyo, Mkuu wa Majeshi nchini, leo tarehe 25 Novemba 2019 katika hafla ya uwekaji jiwe la msingi la ujenzi wa makao makuu hayo, iliyofanyika Kikombo, Wilaya ya Chamwino jijini Dodoma.
Jenerali Mabeyo amesema sehemu ya fedha hizo zitatumika kujenga makao makuu yanayokidhi viwango vya kimataifa, ambapo kutakuwa na ofisi maalumu ya Amiri Jeshi Mkuu wa Nchi, kwa ajili ya kutekeleza majukumu yake ya ulinzi wa taifa.
Mkuu huyo wa Majeshi amesema China imetenga fedha hizo, baada ya Tanzania kuiomba msaada wa kuboresha dhana za jeshi na ujenzi wa makao makuu hayo.
“Ombi la tatu kwa China ilikuwa ni ujenzi wa eneo hili la makao makuu, yanayokidhi viwango vya kimataifa. Kwa maana kwamba, Amiri Jeshi Mkuu anaweza akafanyia kazi hapa, akatekeleza majukumu ya kiulinzi akiwa katika makao makuu ya kiulinzi,” amesema Jenerali Mabeyo na kuongeza;
“Kwa maana unakuwa na ofisi maalumu hapa, ya kutoa maekelezo ya kiulinzi. Naomba nikufahamishe kwamba, marafiki zetu walikubali na kwa sasa hivi tayari wametenga RMB 300 milioni.”
Wakati huo huo, Jenerali Mabeyo amempongeza Rais John Magufuli kwa kuafiki ujenzi wa makao makuu hayo, pamoja na juhudi zake katika kuimarisha utendaji kazi wa majeshi nchini, pamoja na kuboresha maslahi ya askari wa jeshi.
Jenerali Mabeyo amesema Jeshi linamuunga mkono kwa hatua anazochukua.
Leave a comment