HOFU imeanza kukumba vyama vya upinzani nchini, kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika tarehe 24 Novemba 2019. Anaripoti Martin Kamote … (endelea).
Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMMA), kimeitaka Wizara ya Ofisi ya Rais-TAMISEMI kusimamia haki kutokana na kile ilichoita hulka ya CCM kuanza kampeni kabla ya muda wake.
Ombi hilo limetolewa tarehe 23 Oktoba 2019 na Eugine Kabendera, naibu katibu mkuu wa chama hicho Bara, wakati akizungumza na mwandishi wa mtandao huu jijini Dar es Salaam.
Kabendera amesema, baadhi ya vifungu vya kanuni za uchaguzi, havijaweka wazi, vitendo vinavyoashiria kwamba ni kampeni.
“Wagombea wanapatikana zaidi ya siku 10 kabla ya kampeni kuanza, lakini sheria inataka kutoanza kampeni kitu ambacho ni kigumu. Haiwezekani na hatuamini kama CCM wanaweza kutoanza.
“Kura za maoni tu wametoana manundu, sasa wakishapatikana na kujuana kwamba huyu ni fulani, watakaa kimya kwa muda wa siku 12 bila kuanza kujipitisha? Tunahitaji ufafanuzi.”
Kabendera amesema, ni vyema mamlaka husika zitakatoa ufafanuzi huo mapema ili kuondoa sinyofahamu kwa vyama vya siasa, wakati wagombea wao wakisubiri muda wa kampeni.
Pia amesema, chama chake kimejiandaa kushiriki uchaguzi huo, na kutoa wito kwa vyama vya siasa vya upinzani kushiriki pamoja.
“Umoja ni nguvu, utenganbo ni dhaifu na umoja katika kipindi hiki hauepukiki, viongozi wa siasa waone kuna umuhimu wa kuwa na umoja. Ukienda kupigana vita hii peke yako, hatujui nani ataibuka mshindi. Nawasihi wakuu wa vyama walione hilo. Na naamini hivi karibuni viongozi wa vyama watakaa na kujadili,” amesema Kabendera.
Leave a comment