SHUGHULI ya uchukuaji na urudishaji fomu za kugombea urais wa Zanzibar katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020, kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), zitaanza kutolewa kuanza Jumamosi tarehe 4 hadi 19 Julai 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea).
Hayo yamesemwa leo Jumatano tarehe 1 Julai 2020 na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema-Zanzibar, Salumu Mwalimu alipozungumza na waandishi wa habari kuhusu mchakato wa kumpata mgombea urais, ubunge na uwakilishi.
Amesema, mchakato wa uchukuaji na urejeshaji fomu kwa mwanachama wa chama hicho anayetaka kugombea Urais wa Zanzibar utahitimishwa saa 10:00 jioni ya tarehe 19 Juni 2020.
Mwalimu amesema, mtia nia au wakala wake atatakiwa kuchukua fomu za kugombea Urais wa Zanzibar, Ofisi za Makao Makuu ya Chama Zanzibar, Kisiwandui ambazo ni gharama yake ni Sh.1 milioni.
“Kila mgombea atatakiwa kudhaminiwa na angalau wanachama 100 kutoka kila kanda (kanda 2 za Chadema Zanzibar ya Pemba na Unguja),” amesema Mwalimu.
Mwalimu amesema, wadhamini hao wasiwe wajumbe wa mkutano mkuu wa Chama Taifa ambao utafanya uteuzi wa mwisho wa mgombea urais.
Amesema, mgombea au wakala wake, atatakiwa kuwasilisha fomu za kuomba uteuzi pamoja na viambatanisho vyote vilivyotajwa katika fomu na stakabadhi ya malipo ya fomu katika Ofisi ya Makao Makuu ya Chama, Zanzibar, si zaidi ya tarehe 19 Julai, 2020, saa 10.00 jioni.
Mwalimu amesema, Kamati Maaluam ya Zanzibar itakutana tarehe 20 Julai, 2020 kupitia majina ya wogembea na kuwasilisha ripoti yake mbele ya Kamati Kuu ya chama tarehe 22 Julai, 2020.
Amesema, kamati kuu itapendekeza jina au majina ya wagombea kwenda Baraza Kuu na Mkutano Mkuu kwa ajili ya uteuzi wa mwisho kwa mujibu wa Katiba ya Chama ya Mwaka 2006, toleo la mwaka 2019, ibara ya 7.7.12(a) na 7.7.10(c).
Soma zaidi:-
Kuhusu nafasi za uwakilishi wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, Mwalimu amesema, wagombea wote wa nafasi ya uwakilishi watajaza fomu za kuomba uteuzi wa kugombea nafasi hiyo ndani ya chama kwa mujibu wa Kanuni ya 7.2.3 ya Kanuni za Chama.
Amesema, fomu hizo zitakuwa na kipengele cha sifa za mgombea, sambamba na zile zilizoainishwa kwenye Katiba ya Zanzibar, ya mwaka 1984, Toleo la 2010, pamoja na Sheria ya Uchaguzi Nam. 4 ya mwaka 2018.
“Ratiba ya kuchukua, kujaza na kurejesha fomu za kugombea nafasi ya uwakilishi itaanza tarehe 4 Julai, 2020 hadi Julai 10, 2020,” amesema Mwalimu.
Amesema, fomu hizo zitatolewa na Ofisi za Kanda za Chadema katika kanda za Unguja na Pemba. Pia zitapatikana kwenye tovuti ya chama hicho.
Mwalimu amesema,ratiba ya kura za maoni za kamati za utendaji za Chama (Jimbo), chini ya usimamizi wa Kanda, zitaanza tarehe 13 hadi 17 Julai, 2020.
“Kamati Maalum Zanzibar itakutana Julai 25, 2020 kwa ajili ya kupitia majina ya wagombea na kutoa mapendekezo yake kwa Kamati Kuu ya chama itakayokutana tarehe 30 Julai, 2020 kwa ajili ya uteuzi wa mwisho,” amesema
Kuhusu udiwani, Mwalimu amesema utaratibu wa kuwapata wagombea wa udiwani Zanzibar, utaendeshwa kwa kuzingatia ibara ya 7.3.9(a) ya Katiba ya Chama, huku kila mgombea akiitwa mbele ya Kamati ya Utendaji kueleza taarifa zake, kabla ya Mkutano Mkuu wa Kata kuketi na kufanya kura za maoni kwa wagombea wote kwa mujibu wa ibara ya 7.3.7(g).
Amesema, baada ya kamati ya utendaji ya kata kufanya uteuzi wa awali kwa mujibu wa ibara ya 7.3.9(a) na kuwasilisha mapendekezo yake, Kamati ya Utendaji ya Jimbo itafanya uthibitisho wa wagombea udiwani kwa mujibu wa ibara ya 7.4.10(a).
Mwalimu amesema, kwa nafasi ya Udiwani na Uwakilishi wa Viti Maalum, utaratibu ulivyoainishwa kwenye Mwongozo wa Baraza la Wanawake wa Mwaka 2006, Toleo la Mwaka 2019, utafuatwa kwa ukamilifu wake, hatimae uteuzi wa mwisho utafanywa na Kamati Kuu ya Chama kwa vigezo vilivyowekwa na ibara ya 7.4.3 ya Kanuni za Chama.
Leave a comment