SIKU chache baada ya aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu kujivua uanachama wa Chama cha Mapinduzi (CCM) na nafasi yake ya ubunge na kujiunga na Chadema, ameanza kuonja chungu ya uamuzi wake, baada kushutumiwa kwa matumizi mabaya ya madaraka, anaandika Dany Tibason.
Shutuma hizo dhidi ya Nyalandu zimeibuliwa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamis Kigwangalla bungeni leo alipokuwa akichangia Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 207/2018.
Dk Kigwangalla ameiagiza Takukuru na polisi kumchunguza Nyalandu kwa matumizi mabaya ya madaraka ili sheria ichukue mkondo wake.
Waziri huyo amesema Nyalandu alipokuwa waziri aliikosesha serikali mapato ya Sh. 32 bilioni kwa miaka miwili aliyohudumu katika wizara hiyo kwa kushindwa kusaini sheria ya tozo kwa hoteli za kitalii.
Mbali na tuhuma hiyo, pia alimtuhumu kutumia helkopta ya mwekezaji mmoja raia wa kigeni, kipindi cha kampeni zake za kugombea urais 2015, wakati kampuni ya raia huyo ilikuwa ikituhumiwa kwa ujangili.
Nyalandu aliwahi kuliliwa akisema kuwa tuhuma ambazo zimeanza kuibuliwa mitandao dhidi yake si za kweli bali zinalenga tu kumchafua na kuhoji iweje ziibuliwe sasa zaidi ya miaka miwili tangu aachie uwaziri.
Leave a comment