BARAZA la Vijana la Chadema Taifa (Bavicha), limetangaza mgogoro na Jeshi la Polisi Nchini, huku likitoa siku saba kwa Mkuu wa Jeshi hilo (IGP), kutoa kauli kama kuwapo kwa vyama vingi nchini ni kosa la jinai au la, vinginevyo wataandamana nchi nzima, anaandika Hamisi Mguta.
Patrobas Katambi, Mwenyekiti wa Baraza la Vijana la chama hicho, (BAVICHA), amesema kama itafika wiki ijayo hawajapata majibu watafanya maandamano Agosti 31, mwaka huu siku ya Alhamisi. Maandamano hayo wametapa jina ‘Black Thursday’.
BAVICHA wamesema maandamano hayo ya amani yatalenga kushinikiza kuwapo haki za kisiasa, kiuchumi, utawala wa sheria, na haki za binadamu.
Baraza hilo limesema kuwa kuna watu wametenda matendo mabaya katika nchi hii yakiwamo ya wizi wa fedha za umma lakini wapo huru, lakini viongozi wa Chadema wanaosema ukweli wanakamatwa kila siku.
Hii ni mara ya pili kwa upinzani kutaka kuandamana nchi nzima, mara ya kwanza waliweka nia ya kuandamana baada ya uchaguzi mkuu mwaka 2015, kupinga udikteta na kuyaita maandamano hayo kama UKUTA.
Hata hivyo, Ukawa waliahirisha na kutangaza kuyafanya siku nyingine jambo ambalo halijafanyika mpaka leo.
Leave a comment