MKURUGENZI wa Mambo ya Nje, Mawasiliano na Uenezi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), John Mrema, amedai kuwa wabunge wake waliofukuzwa wana haki ya kukata rufaa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
“Katiba yetu inatoa haki kwa mwanachama kukatia rufaa uamuzi uliotolewa ndani ya siku 14 tangu uamuzi huo ulipotolewa. Wanachotakiwa walalamikaji, ni kueleza sababu za rufaa yao ndani ya chama,” amesema Mrema.
Ameongeza: “Jambo ambalo hatuliewi ni kwa nini, wahusika wamewasilisha rufaa yao kwa Msajili wa Vyama, badala ya kupeleka ndani ya chama.”
Alipoulizwa iwapo chama chake, kiliwaita wahusika kabla ya “kuwahukumu,” Mrema alisema, “nisingependa kuingilia ‘process’ ya rufaa iliyokwisha kukatwa.”
Amesema, “kama chama kwa sasa, hatutakuwa na la kusema. Tunasubiri hiyo rufaa isikilizwe na kama watasema hawakuhojiwa, tutakuwa na la kusema.”
Chadema kupitia kikao chake cha Kamati Kuu (CC), kiliamua kuwavua uwanachama wabunge wake wanne mashuhuri, kwa kile walichoita, “kukaidi maelekezo ya chama.”
Wabunge waliofukuzwa, ni Wilfred Muganyizi Lwakatare (Bukoba Mjini); Anthony Calist Komu (Moshi Vijijini); David Silinde (Momba) na Joseph Selasini (Rombo).
Tayari Lwakatare, Komu, Selasini na Silinde, wamewasilisha rufaa yao kwa Msajili wa Vyama vya siasa, kupinga uamuzi wa kuwafukuza uwanachama.
Kauli ya Chadema imekuja siku mbili, tangu wabunge hao kuwafukuza ndani ya chama hicho kuanzia tarehe 11 Mei mwaka huu.
Kikao cha CC kilichofanyika kwa siku mbili, chini ya uenyekiti wa Freeman Mbowe, kiliamua kuwavua uwanachama wabunge hao, “pasi na kuwasikiliza.”
Katiba ya Chadema inaruhusu kila mwanachama asiyeridhika na maamuzi ya kikao kilichomtia hatiani, kukatia rufaa uamuzi huo, ndani ya siku 14.
Kupatikana kwa taarifa hizi kumekuja siku moja tokea Prof. Abdallah Safari, ambaye amepata kuwa Makamu Mwenyekiti wa taifa wa Chadema, kukosoa maamuzi hayo.
Akizungumza na MwanaHALISI jijini Dar es Salaam, Prof. Safari alisema, “Katiba ya Chadema inapiga marufuku mtu yeyote kuhukumiwa bila kupewa nafasi ya kujitetea.”
Aliongeza: “Haya yanakatazwa na hata Katiba ya Nchi na kwamba sheria zinaeleza wazi, kwamba mtu ambaye hakupewa haki ya kujitetea, uamuzi huo ni batili.”
Akizungumza na mwandishi habari hizi juzi Alhamisi, Komu alisema, wameamua kukata rufaa kwa Msajili kwa kuwa vikao vinavyotakiwa kufanyia maamuzi rufaa yao, vitaongozwa na mtu yuleyule ambaye amefanya maamuzi ya kuwafukuza na ambaye kimsingi ndiye mlalamikaji katika kesi hiyo.
Msajili wa vyama vya siasa, Jaji Francis Mutungi alishathibitishia MwanaHALISI ONLINE kwamba barua hizo za rufaa zimefika ofisini kwake na anazifanyia kazi.
Leave a comment